Mahakama ya Juu ya Iran imekubali rufaa ya waandamanaji wawili waliohukumiwa kifo Mahakama ya Juu ya Iran imekubali rufaa ya waandamanaji wawili waliohukumiwa kifo
Mahakama ya Juu ya Iran imekubali rufaa ya waandamanaji wawili waliohukumiwa kifo kutokana na dosari katika uchunguzi wa kesi zao. Kwa mujibu wa shirika la habari la mahakama Mizan, Mahakama imekubali rufaa ya watuhumiwa Mohammad Qobadloo na Saman Saidi Yasin. Qobadloo alishtakiwa kwa kumuua ajenti wa polisi na kuwajeruhi wengine watano wakati wa maandamano na Yasin, Mkurdi msanii wa kufokafoka anayeimba kuhusu ukosefu wa usawa, ukandamizaji na ukosefu wa ajira, alishutumiwa kwa kujaribu kuua vikosi vya usalama na kuimba nyimbo za mapinduzi.Mapema mwezi huu Iran iliwanyonga waandamanaji wawili Mohsen Shekari mwenye umri wa 23, aliyeshitakiwa kwa kufunga barabara kuu mwezi Septemba na kumjeruhi mwanajeshi wa jeshi la Basij kwa kisu. Na Majid Reza Rahnavard, mwenye umri wa miaka 23, kwa kuwachoma kisu wanachama wawili wa Basij, alinyongwa hadharani.
China yapuuzilia mbali mswada wa ulinzi wa Marekani
China imepuuzilia mbali mswada wa kila mwaka wa matumizi ya ulinzi wa Marekani kwa kuibua hoja kuwa China ndio tishio kubwa.Taiwan imesifu hatua hiyo. Imsema kwamba Marekani imeonyesha uungaji mkono wa kisiwa hicho kinachojitawala ambacho China inasema lazima kiwe chini ya utawala wake. Kupitia taarifa iliyochapishwa mtandaoni Waziri wa mambo ya nje wa China amesema, China inachukia na inapinga vikali hatua ya Marekani akitaja sheri hiyo mpya kama uchochezi mkubwa wa kisiasa ambao unaingilia waziwazi mambo ya ndani ya China. Rais Joe Biden alitia saini mswada wa ulinzi wa dola bilioni 858 kuwa sheria mjini Washington siku ya Ijumaa. Mswada huo unajumuisha takriban dola bilioni 45 kukabiliana na mfumuko wa bei na kuongeza ushindani wa kijeshi wa dhidi ya China na Urusi.
Zaidi ya watu milioni 200 watahadharishwa kuhusu baridi kali Marekani
Shirika la taifa la utabiri wa hali ya hewa nchini Marekani, limetoa tahadhari kwa zaidi ya watu milioni 200 kuhusu hali ya baridi kali inayokumba nchi hiyo katika kipindi hiki cha sikukuu. Wataalam wa hali ya hewa wameonya kwamba kutokana na baridi kali mtu anaweza kudhurika kwa dakika chache kwa kupoteza joto mwilini. Umeme umekatika katika baadhi ya maeneo na kuwaathiri zaidi ya watu milioni moja hasa pande za kusini na mashariki mwa taifa hilo. Hapo jana watu wawili waliripotiwa kufariki kufuatia ajali ya barabarani jimbo la Oklahoma na katika jimbo la Kansas watu watatu pia walifariki kufuatia ajali ya barabarani. Zaidi ya safari 3,250 za ndege zimefutwa na nyingine 1,900 zimecheleweshwa kufuatia hali hiyo ya hewa.
Burkina Faso yamfukuza afisa mwandamizi wa Umoja wa Mataifa
Serikali ya kijeshi ya Burkina Faso imemuamuru mratibu wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa, Barbara Manzi, kuondoka nchini humo mara moja. Taarifa ya wizara ya mambo ya kigeni imetangaza kwamba Manzi mkazi wa Umoja wa Mataifa na msaidizi wa masuala ya kibinadamu katika taifa hilo la Afrika Magharibi kuwa mtu asiyefaa. Ingawa hakuna sababu iliyotolewa katika taarifa ya kufukuzwa kwake, Waziri wa mambo ya nje Olivia Rouamba alisema kwenye televisheni ya taifa siku ya Ijumaa kuwa Manzi alikuwa ametoa tahadhari kuhusu ukosefu wa usalama katika mji mkuu, Ouagadougou, bila kutoa ushahidi. Takriban watu milioni mbili hawana makaazi nchini humo na wanaishi katika kambi, ambazo nyingi yao zinaendeshwa na Umoja wa Mataifa.
Kansela Scholz alaani ufyatuaji risasi 'mbaya' huko Paris
Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amelaani "kitendo kibaya" cha mtu aliyekuwa na bunduki kufyatua risasi katika kituo cha kitamaduni cha Kikurdi huko Paris Ufaransa na kilichosabisha kifo cha watu watatu na wengine watatu kujeruhiwa. Rais Emmanuel Macron alisema jamii ya Wakurdi nchini Ufaransa imekuwa ikilengwa katika shambulio hilo, huku waziri wa mambo ya ndani ya Ufaransa Gerald Darmanin akisema mshukiwa wa shambulizi hilo alikuwa akilenga wageni. Maafisa walisema wamemkamata mzee wa miaka 69, ambaye Mwendesha mashtaka wa Paris Laure Beccuau alisema alikuwa ameachiliwa hivi karibuni kizuizini wakati akingojea kesi kwa shambulio jengine katika kambi ya wahamiaji huko Paris mwaka mmoja uliopita. Askari wa kutuliza ghasia walifyatua vitoa machozi kutawanya umati wa watu wenye hasira uliokusanyika karibu na eneo la tukio.
Watu 20 wamekufa kwa moto katika nyumba ya wazee Urusi
Watu 20 wamefariki katika ajali ya moto katika kituo cha kulea wazee katika mji wa magharibi wa Siberia wa Kemerovo. Kulingana na maafisa wa ulinzi wa raia, moto huo ulizuka usiku wa kuamkia leo katika jengo hilo huku picha na video zilizotolewa na mamlaka zilionyesha jengo hilo likiteketea na kuharibika. Watu wawili walipelekwa hospitalini wakiwa na majeraha ya moto. Uchunguzi unaendelea kuhusu ukiukaji wa kanuni na usalama wa moto katika kituo hicho ambacho kilianzishwa katika jengo la kibinafsi.Shirika la habari la TASS limeripoti kwamba mmiliki wa jengo hilo na mchungaji anayedaiwa kuendesha kituo hicho wamehojiwa na kubaini kwamba kituo hicho hakina vibali vinavyohitajika. Chanzo cha moto huo kinashukiwa kuwa ni matumizi yasiyofaa ya jiko.Wizara ya Ulinzi wa Raia ilisema afisa wa usalama wa moto alipangiwa kukagua kituo hicho Desemba 7 lakini hakuruhusiwa katika kituo hicho.
Watu saba wameuwawa katika mapigano Dafur
Mapigano kati ya makundi ya Kiarabu na yasiyo ya Kiarabu katika jimbo la Darfur nchini Sudan yamesababisha vifo vya takriban watu saba. Taarifa ya vyombo vya habari vya serikali imeripoti kwamba ghasia zilizuka siku ya Jumatano karibu kilomita 20 kutoka mji mkuu wa jimbo la Darfur Kusini Nyala kati ya wafugaji wa Kiarabu dhidi ya wakulima kutoka jamii ya wachache ya Daju na makabila mengine yasiyo ya Kiarabu. Hata hivyo haijabainika mara moja nini kilichochea mapigano hayo. Mapigano ya kikabila mara nyingi huzuka huko Darfur, eneo liliharibiwa na vita vikali vya wenyewe kwa wenyewe vilivyozuka mwaka wa 2003. Mzozo huo uliwakutanisha waasi wa makabila madogo dhidi ya serikali iliyotawaliwa na Waarabu ya rais wa wakati huo Omar al-Bashir. Kulingana na Umoja wa Mataifa takriban watu 300,000 waliuawa na milioni 2.5 kukimbia makazi yao.