1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika Kusini yatuma Wanajeshi kwa waathirika wa mafuriko

Hawa Bihoga
20 Aprili 2022

Idadi ya watu waliopoteza maisha katika mafuriko hayo imefikia kiasi cha watu 448, huku zaidi ya 40,000 wakikosa makaazi, miundombinu ya umma zikiwemo shule na hata vituo vya afya vimeharibiwa vibaya.

Südafrika Kapstadt | Brand im Parlament
Picha: Sumaya Hisham/REUTERS

Takriban wanajeshi 10,000 wa Afrika Kusini wanatarajiwa kuingia katika eneo la pwani la KwaZulu-Natal leo Jumatano, kusaidia kusafisha baada ya dhoruba kubwa iliosababisha vifo vya watu 448 wiki iliopita.

Rais Cyril Ramaphosa ametangaza hali ya dharura kitaifa kutokana na dhoruba hiyo ambayo hadi sasa bado makumi ya watu hawajulikani walipo.

Kwa mujibu wa maafisa wa serikali takriban watu 40,000 hawana makaazi kutokana na mafuriko hayo, yaliosababishwa na mvua ilionyesha kwa kiwango cha milimita 400 huko katika eneo la KwaZulu-Natal ndani ya saa 24.

Hiki ni kiwango chake cha kawaida cha mvua kwa mwaka mzima. baadhi ya maeneo hayana umeme wala maji salama.Durban mojawapo ya bandari kubwa zaidi barani Afrika imefungwa.

Soma zaidi:Watu 443 wafa katika mafuriko ya Afrika Kusini

Miundombinu ikiwemo shule 630, vituo vya afya 84, nyumba, mitaa na madaraja yanatarajiwa kufanyiwa matengenezo yatakayogharimu mamia kwa mamilioni ya dola.

Mamilioni yatengwa kurejesha miji katika hali ya kawaida

Mkoa huo ulikuwa unafanyiwa matengenezo yaliogharimu mamilioni ya dola baada ya maandamano makubwa ya kisiasa na uporaji mwezi Julai.

Kadhalika ni maeneo muhimu kwa mapumziko na ilijiandaa kupokea wageni mwaka huu baada ya miaka miwili ya kupungua umati wa watu kutokana na janga la Corona.

Ramaphosa asema atakomesha machafuko Afrika Kusini

01:20

This browser does not support the video element.

Baada ya kushuhudiwa kwa mafuriko hayo mabaya zaidi kutokea, Rais Cyril Ramaphosa ametangaza hali ya dharura kwa taifa kutokana na dhoruba hiyo na kuelezea namna serikali itakabiliana na janga hilo ikilenga katika kusaidia waathiriwa kadhalika   kujenga upya miundombinu.

Rais Ramaphosa aliongeza kuwa ufisadi hautavumiliwa katika kipindi hiki cha kukabiliana na maafa."tutalishughulikia janga hili kwa awamu tatu,mosi tutazingatia misaada ya haraka ya kiutu" Alisema huku akionesha namna seriklali yake itakavyoshughulikia janga hilo.

"Tutazingatia uimarishaji na urejeshaji wa nyumba, kuwaweka upya watu ambao wamepoteza makazi na kurejesha utoaji wa huduma." Alisema katika hotuba yake kwa taifa

Soma zaidi:Idadi ya waliokufa mafuriko Afrika Kusini yakaribia 400

Nchi hiyo imetenga dola milioni 67 kusaidia walioathiriwa na mafuriko ambayo yamesababisha vifo vya takriban watu 448 katika mji wa mashariki wa Durban na jirani wa KwaZulu-Natal.

Jitihada za kutoa misaada za kiutu zaendelea

wanajeshi hao wanatarajiwa kuendeleza juhudu za raia na makundi ya kiraia katika juhudi za utafutaji na uokoaji wa watu, kupeleka chakula,maji na nguo kwa waathirika wa mafuriko.

Raia akiwa na ndoo za maji safi yaliotolewa na serikaliPicha: PHILL MAGAKOE/AFP

Mapipa ya maji safi yamepekwa katika maeneo ambayo upatikanaji wa maji salama umetatizika huku timu nyingine ikafanya kazi kurejesha umeme.

 Afrika Kusini ilikuwa katika hali ya maafa ya kitaifa kutokana na COVID-19 tangu Machi 2020 hadi ilipoondolewa wiki mbili zilizopita, lakini sasa imerejeshwa katika kukabiliana na mafuriko.

Soma zaidi:Mvua kubwa yaendelea kuipiga Afrika Kusini

Tangu mwaka uliopita bara la Afrika  limekuwa likishuhudia mfululizo wa changamoto kadhaa kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa.

Mafuriko yanayoendelea kushuhudiwa katika maeneo kadhaa, vimbunga visivyoisha katika upande wa kusini, joto kali katika ukanda wa magharibi na kaskazini na hata ukame unaosumbua mashariki ya kati na pembe ya Afrika.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW