Xabi Alonso akabiliwa na shinikizo kufuatia kipigo
11 Desemba 2025
Kocha wa Real Madrid Xabi Alonso amewashukuru wachezaji wake kwa kujituma uwanjani licha ya kipigo cha mabao 2-1 mbele ya Manchester City katika mechi ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya iliyochezwa uwanjani Santiago.
Alonso amesema anaamini klabu hiyo itarejea kwenye kiwango chake cha kawaida hivi karibuni.
Miamba hao wa Uhispania wamepata ushindi katika mechi mbili pekee kati ya nane zilizopita katika mashindano yote.
Matokeo hayo yameongeza shinikizo kwa Alonso huku vyombo vya habari nchini humo vikiripoti juu ya kuwepo kwa mgawanyiko kati ya kocha huyo na baadhi ya wachezaji wake, ingawa wachezaji kadhaa wamejitokeza hadharani na kuonyesha kumuunga mkono.
Kwengineko, klabu inayoshiriki ligi kuu ya Ujerumani Bundesliga, Bayer Leverkusen imetoka sare ya 2-2 na Newcastle United katika mchezo wa kusisimua wa Ligi ya Mabingwa barani Ulaya.
Alejandro Grimaldo alifunga bao dakika ya 88 ya mchezo na kuhakikisha wanagawanya alama na Newcastle.