1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bado ukiukwaji wa haki za binadamu unaendelea Darfur

Saumu Mwasimba24 Septemba 2007

Ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu unaendelea kufanyika katika jimbo la Darfur magharibi mwa Sudan kwa mujibu wa Umoja wa mataifa.

Picha: AP

Kundi la wataalamu wa Umoja wa mataifa wanaoangalia hali katika jimbo hilo wamesema hayo katika ripoti yao.

Katika ripoti iliyotolewa kwa baraza la usalama la Umoja wa mataifa,wataalamu hao wasema serikali ya Sudan inateleza baadhi ya mapendekezo yao kuzuia ukiukaji wa haki za binadamu kwenye jimbo hilo ijapokuwa hatua iliyopigwa sio ya kuridhisha.

Wataalamu hao wa Umoja wa mataifa wamesisitiza juu ya wasiwasi wao kuhusu taarifa za kuendelea kukiukwa kwa sheria ya kimataifa juu ya haki za binadamu kunakofanywa na makundi mbali mbali yanayohusika katika mgogoro wa jimbo la Darfur.

Kutokana na hali hii wataalamu hao wameitaka serikali ya mjini Khartoum kulishughulikia suala hilo na kuhakikisha wahusika wa vitendo vya ukiukaji haki za binadamu wanachukuliwa sheria.Hata hivyo wataalamu wa Umoja wa mataifa hakutoa orodha ya matukio ya ukiukaji huo wa haki za binadamu.

Mkuu wa Umoja wa mataifa anayehusika na masuala ya kutetea haki za binadamu Loiuse Arbour wiki iliyopita pia alitahadharisha juu ya ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanyika Darfur akisema bado kiwango cha unyanyasaji katika eneo hilo kiko palepale.

Aidha alisema dalili ni ndogo mno kwamba serikali ya Sudan ina nia ya kuitikia warranti za kukamatwa wahusika wa vitendo hivyo zilizotolea na mahakama ya kimataifa inayoshulikia makosa ya uhalifu.

Mjumbe wa Umoja wa mataifa Walter Kaelin ambaye ni miongoni mwa kundi la wataalamu wa Umoja huo walioko Darfur ameipongeza serikali ya Sudan kwa kutoa ushirikiano pamoja na kutia juhudi katika kuhakikisha utekelezwaji wa hatua za kukomesha vitendo vya uonevu jimboni humo.

Pamoja na hayo lakini mjumbe huyo ameweka bayana kwamba mapendekezo machache yaliyotekelezwa na serikali ya Sudan kundi lake haliwezi kusema kuwa hali ni nzuri katika eneo la mgogoro. Ameongeza kusema wataalamu hao wanataka kuipa muda wa kutosha serikali ya Sudan kutimiza wajibu wake na hivyo tathmini kamili juu ya hali ya mambo jimboni Darfur itatolewa mwezi Desemba.

Ujumbe wa Sudan katika baraza la usalama la Umoja wa Mataifa umekubaliano na ripoti ya wataalamu wa Umoja huo.

Itakumbukwa kwamba mwezi Juni wataalamu wa Umoja wa mataifa walitoa mapendekezo zaidi ya 30 kwa Sudan ikiwa ni pamoja na sharti la wazi la kutaka mashambulizi dhidi ya raia yakomeshwe, kupokonywa silaha waasi na pia serikali ya Sudan ishirikiane kikamilifu na mahakama ya ICC.

Kwa upande mwingine wataalamu hao wamekiri kwenye ripoti yao kwamba kuongezeka kwa makundi yanayozozana kunatatiza juhudi za kuweka sawa hali ya mambo jimboni Darfur lakini wameonya kwamba makundi hayo hayawezi kuitwa ni kipingamizi katika kuzuia uvunjwaji sheria.

Makundi ya waasi katika jimbo la Darfur yamegawika katika makundi mbali mbali baadhi yanapinga makubaliano ya amani na yamegawika juu ya kufanyika mazungumzo zaidi na serikali ya Khartoum mwezi ujao.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW