1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern yaporwa ushindi na Freiburg

Sekione Kitojo
5 Novemba 2018

Freiburg yaipokonya Bayern pointi mbili  muhimu, Hoffenheim yapiga breki ushindi mfululizo wa Bayer Leverkusen  na  Borussia  Dortmund bado  iko kileleni mwa  msimamo wa  ligi ya  Bundesliga.

Bundesliga 10. Spieltag | FC Bayern München vs. FC Freiburg | 
Wachezaji wa SC Freiburg wakimwangalia Robert Lewandowski wa Bayern Munich na mpiraPicha: Reuters/A. Gebert

Kwa  shuti  moja  tu  kuelekea  golini  SC Freiburg  ilifanikiwa  siku ya  Jumamosi  kuikaba  koo  Bayern  Munich  na  kutoka  nayo  sare ya  bao 1-1  katika  uwanja  wa  Alianz Arena  mjini  Munich, ikiwa ni mara  nyingine  tena  kikosi  hicho  cha  kocha  Nico Kovac kuonesha  mchezo  dhaifu, na  kuendeleza  mjadala  juu  ya  uwezo wa  kocha  huyo  katika  kikosi  cha  Bayern.

Wachezaji wa Bayern Munich wakilalamika kwa mwamuzi Picha: Reuters/A. Gebert

Matokeo  hayo yanaiweka  Bayern  Munich  mabingwa  watetezi  wa  Bundesliga msimu  kuwa  nyuma  ya  Borussia  Dortmund kwa  pointi  nne. Borussia  Dortmund  ilifanikiwa  kupata  ushindi  mwembamba  wa bao 1-0 mbele  ya  VFL Wolfsburg, ikijipasha  joto  kwa  pambano lao  mwishoni  mwa  juma.

Borussia  Dortmund  inakaribisha  Bayern Munich siku  ya  Jumamosi  katika  pambano  la  el Classico  nchini Ujerumani.

Bayer 04 Leverkusen  ililazimishwa  kupiga  magoti mbele  ya Hoffenheim  baada  ya  kucharazwa  kwa  mabao 4-1 nyumbani, kipigo  ambacho  kimesimamisha matumaini  ya ushindi  mfululizo  wa Leverkusen katika  Bundesliga  baada  ya  kuitwanga  Werder Bremen mabao 6-2 katika mchezo wa  wiki  ya  9  ya  Bundesliga na pia  ushindi  wa  mabao 5-0 dhidi  ya  Borussia  Moenchengladbach katika  kombe  la  shirikisho DFB Pokal .

Kikosi cha Borussia Dortmund wakimshangilia Marco Reus baada ya kufunga baoPicha: Reuters/F. Bimmer

Katika  msimamo  wa  ligi kuna  mvutano  mkubwa  kuelekea kuwania  nafasi  nne  za  juu  ili  kucheza  katika  Champions League msimu  ujao, pamoja  na  Europa league.

Borussia  Dortmund  iko kileleni  ikiwa  na  pointi 24 , wakati  Borussia  Moenchenglandbach iko katika  nafasi  ya  pili  ikiwa  na  pointi  20 , sawa  na  Bayern Munich  iliyoko  katika  nafasi  ya  tatu, na  inafuatiwa  na  RB Leipzig  yenye  pointi 19, timu  hizo  tatu zikipishana  tu kwa  pointi moja.

Timo Werner (11) akipachika bao dhidi ya Hertha BerlinPicha: Imago/Contrast/O. Behrendt

Eintracht Frankfurt iko  katika  nafasi  ya  tano  ikiwa  na  pointi 17 sawa  na  Werder  Bremen , na TSG Hoffenheim  iko  katika nafasi  ya  7  ikiwa  na  pointi 16 sawa  na  Hertha  Berlin.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe / ape / dpae / rtre

Mhariri: Mohammed  Abdul-Rahman

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW