1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Berlin yajiandaa kwa uchaguzi wa kurudiwa

8 Februari 2023

Msukosuko ambao haukutarajiwa wa uchaguzi wa Berlin Septemba 2021, uligonga vichwa vya habari kimataifa. Sasa mji huo mkuu Ujerumani unajiandaa kurudia uchaguzi huo maafisa wakijaribu kurejesha imani iliyovunjika.

Deutschland | Wiederholungswahlen in Berlin
Picha: Jens Kalaene/dpa/picture alliance

Mji wa Berlin utafanya uchaguzi wa kurudiwa wa jimbo hilo Jumapili. Wengi wanatizama hali hiyo ambayo haijawahi kutokea ya kurudiwa kwa uchaguzi kuibua maswali juu ya uaminifu wa taasisi za kidemokrasia za Ujerumani.

Maafisa katika mji mkuu wa Ujerumani Berlin, wamekuwa chini ya uchunguzi zaidi tangu Novemba mwaka jana, wakati mahakama ya kikatiba ilipobatilisha uchaguzi uliofanywa Septemba 26 mwaka 2021 wa jimbo na hilo na manispaa, na kutoa uamuzi uliosema uchaguzi huo ulishughulikiwa vibaya.

Kuchelewa kwa vifaa vya uchaguzi kulisababisha watu kusubiri kwa saa nyingi kwenye foleni. Katika vituo vingine karatasi za kura zilikwisha na kulazimisha maafisa kutoa nakala zaidi. Karatasi nyingine zilikuwa na dosari za wagombea waliochapishwa. Vituo vingine vililazimika kufunga kwa muda na vingine vilihudumu kupita muda vilipaswa kufungwa. Wakati huo huo, mbio za marathon za jiji hilo zilizofanyika siku hiyo hiyo zilitatiza juhudi za kusambaza vifaa zaidi vituoni.

Uamuzi wa mahakama, matatizo yaliathiri uchaguzi wa asilimia 60 ya viti

Kwa ujumla, mahakama ilisema matatizo hayo yaliathiri uchaguzi wa takriban asilimia 60 ya viti katika bunge la jimbo hilo. Japo hakukuwa na madai ya kuwepo makosa, hali hiyo ilikuwa ya aibu kubwa kama tu ambavyo wanasiasa wengi wamesema.

Maoni: Mwaka mmoja wa Scholz uongozini, sifa zapiku ukosoaji

Meya wa Berlin Franziska Giffey anatumai ataibuka mshindi kuweza kubakia ofisini.Picha: Emmanuele Contini/imago images

Stephen Bröchler, profesa wa utawala wa kisiasa aliyeteuliwa kuwa mkurugenzi mkuu mpya wa uchaguzi uliofanyika Oktoba mwaka uliopita amesema kwa kawaida wanapaswa kuwa na mwaka mmoja wa kuandaa uchaguzi. Lakini mahakama iliwapa muda wa siku 90 pekee. Akizungumza na DW ameelezea walivyojiandaa amesema "inaonekana kuwa jambo lisiloeleweka, lakini miongoni mwa kazi zangu za mwanzo ilikuwa kuhakikisha tuna karatasi za kutosha za kutengeneza kura. Na tumeongeza idadi ya vituo vya kura. Kutakuwa na angalau maeneo matatu ya kupiga kura katika kila kituo. Mwaka 2021, tulikuwa na maeneo mawili".

Marie Jünemann, afisa wa shirika lisilo la serikali kwa jina 'Demokrasia Zaidi' alikaribisha kuteuliwa kwa Bröchler na juhudi zake hadi sasa. Mkurugenzi mtendaji huyo wa uchaguzi ameweka hali ya uwazi kuhusu anavyoshughulikia masuala ya uchaguzi, na kueleza ni kwa nini wanafanya baadhi ya maamuzi.

"Anategemea zaidi uwazi wake, na hiyo ni vizuri. Kuhusu swali kuu la ni kwa nini hakuna anayechukuwa wajibu wa kisiasa, bila shaka mkurugenzi wa zamani alijiuzulu, lakini kwa wakati huo, hakukuwa na shuruti kwa maafisa wa kisiasa mfanbo katika wizara ya Mambo ya Ndani kuwajibika," ameliambia DW.

Yaliyotokea kwenye uchaguzi huo yalikuwa aibu kubwa kwa Ujerumani

Stephan Bröchler, Profesa wa utawala w akisiasa na pia mkurugenzi mpya wa tume ya uchaguzi Ujerumani anaamini kila kitu kitaenda shwari.Picha: Jörg Carstensen/dpa/picture alliance

Haijawahi kutokea uchaguzi kufanyika vibaya nchini Ujerumani kiasi hicho cha kulazimisha urudiwe.

Masuala ya kisheria hayajatatuliwa yote. Lakini wiki iliyopita mahakama ya kikatiba ya shirikisho ilitupilia mbali ombi la kutaka uchaguzi huo usimamishwe.

Mahakama hiyo pia iliahirisha kutoa uamuzi wa mwisho hivyo kufungua uwezekano wa uchaguzi huu mpya pia kubatilishwa.

Aidha bado kuna swali linaloning'inia kuhusu uchaguzi wa shirikisho uliofanyika siku hiyohiyo. Mwaka uliopita, bunge la shirikisho Bundestag, liliamua kwamba uchaguzi utarudiwa katika vituo 431 kati ya jumla ya vituo 2, 256 vya Berlin. Lakini bado haifahamiki waziwazi nini itafanyika, kwa kuwa uamuzi huo unategemea rufaa iliyowasilishwa katika mahakama ya kikatiba ya shirikisho.

Kisiasa, msukosuko huo wa uchaguzi unaonekana kuwa mbaya kwa Meya Franziska Giffey wa Berlin ambaye ni Msoshial Demokrat, ambaye sasa kulingana na uchunguzi wa maoni, amejikuta nyuma ya mpinzani wake kutoka chama cha kihafidhina Christian Democratic Union (CDU).

Mwandishi: Ben Knight

Tafsiri: John Juma

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW