1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BERLIN:Ujerumani yawataka wataleba kumwachia raia wake

24 Julai 2007

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Frank Walter Steinmeir kwa mara nyingine tena amewaomba wateka nyara nchini Afghanistan kumwachia huru Injinia wa kijerumani wanayemshikilia.

Waziri Steinmeir amesema kuwa Ujerumani inashirikiana na Serikali ya Afghanistan kuhakikisha kuwa mjerumani huyo anaachiwa.

Wakati huo huo wateka nyara hao wa Kitaleban wametoa muda zaidi kwa Serikali ya Korea Kusini kutimiza masharti ya kuondoa majeshi yao nchini Afghanistan.

Wataleban hao wanawawashikilia mateka raia 23 wa Korea Kusini na wametoa muda wa saa 24 kabla ya kutimizwa kwa masharti yao vinginevyo watawaua.

Korea Kusini ina askari 200 nchini Afghanistan wanaoshirikiana na jeshi la NATO.

Hayo yakiendelea bomu lililotegwa pembezoni mwa barabara limewaua wanajeshi wanne wa Marekani huko katika jimbo la mashariki mwa Afghanistan la Paktika.

Aidha wanajeshi wengine wawili wa NATO mmoja kutoka Norway waliuawa katika shambulizi la wataliban huko huko Afghanistan na kufanya idadi ya wanajeshi wa jeshi hilo la NATO waliyouawa mwaka huu nchini humo kufikia 114.

Kwa upande wake majeshi hayo ya NATO yanayoongozwa na Marekani yamesema kuwa yamewaua wanamgambo wa kitaleban 60 katika jimbo la kusini la Helmand.

Mjini Kabul, serikali ya Afghanistan inaomboleza kifo cha mfalme wa zamani na wa mwisho wa nchi hiyo Mohammed Zahir Shah aliyefariki jana akiwa na umri wa miaka 92.

Shah alirejea nchini humo mwaka 2002 baada ya kuishi uhamishoni nchini Italia kwa muda wa miaka 30 na alipewa hadhi ya kuwa baba wa taifa la Afghanistan