1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bobi Wine aondosha kesi ya kupinga ushindi wa Museveni

22 Februari 2021

Aliyekuwa mgombea urais nchini Uganda Robert Kyagulanyi amesema hatababaishwa na mawakili wa rais Museveni wanaotaka agharamie hatua yake ya kuondoa kesi ya kuoinga matokeo ya rais aliyowasilisha katika mahakama ya juu.

NUP Präsident Robert Kyagulanyi
Picha: Emmanuel Lubega/DW

Robert Kyagulanyi almaarufu Bobi Wine aliwasilisha kesi katika mahakama ya juu tarehe mosi mwezi huu akipinga hatua ya rais Museveni kutangazwa kuwa mshindi wa uchaguzi wa rais uliopita, kwa kupata asli mia 58 ya kura dhidi yake ambaye alitangazwa kupata asli mia 35 hivi.

Katika kipindi cha wiki mbili amewasilisha shauri katika mahakama hiyo akitaka kuongeza ushahidi zaidi ambao anaelezea ungeweka bayana malalamiko yake kwamba palitokea udanganyifu mkubwa katika uchaguzi sambamba na kutokuwepo na usawa katika mchakato wote wa uchaguzi. Ila mahakama hiyo ilitupilia mbali maombi yake.

soma zaidi:Bobi Wine awasilisha mahakamani rufaa iliyorekebishwa

Ni kwa msingi huu ndipo ameelezea kuwa hana imani na mahakama hiyo kutoa maamuzi ya haki pamoja na kumtaja jaji mkuu kudhihirisha kuwa hawezi kufikia maamuzi kwamba rais Museveni si mshindi halali.

Bobbi Wine kuweka hadharani ushahidi uliokataliwa na mahakama ya juu

Rais wa Uganda Yoweri Museveni na Kiongozi wa upinzani Robert Kyagulanyi

Bobi Wine ameongezea kuwa atauweka wazi kwa umma ushahidi uliokataliwa ili wafahamu kwa nini mahakama hiyo pamoja na upande wa rais Museveni walipinga  kuwasilishwa kwake katika kufikia maamuzi ya kesi hiyo.

soma zaidi:Museveni ashinda muhula wa sita madarakani

Mara tu baada ya kupokea habari za Bobi Wine kuondoa kesi hiyo, wakili Oscar Kihika ambaye anaongoza timu ya mawakili wa chama cha NRM pamoja na rais Museveni ameonya kuwa mwanasiasa huyo atajutia gharama atakazotakiwa kuwafidia kwa hatua hiyo.

Hata hivyo, Bobi Wine amesisitiza kuwa hatababaishwa na mawakili hao na yuko tayari kwa chochote kitakachotokea.

Mwandishi: Lubega Emmanue DW Kampala

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW