1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Marekani lafikia makubaliano

17 Oktoba 2013

Serikali ya Marekani imefungua milango yake leo(17.10.2013) baada ya bunge kupitisha sheria inayomaliza kufungwa shughuli za serikali na kuepusha dakika za mwisho nchi hiyo kushindwa kulipa madeni yake.

Obama hält Rede zur Lage der Nation. United States President Barack Obama delivers his State of the Union Address to a Joint Session of Congress in the U.S. Capitol in Washington, D.C. on Tuesday, January 25, 2011..Credit: Ron Sachs / CNP.(RESTRICTION: NO New York or New Jersey Newspapers or newspapers within a 75 mile radius of New York City)
Bunge la MarekaniPicha: picture-alliance/dpa

Hata hivyo shirika la fedha la kimataifa IMF limeitolea mwito Marekani kufanyakazi zaidi kuweza kudhibiti matumizi ya serikali.

Baraza la seneti lilipiga kura kuidhinisha hatua hiyo kwa kura 81 za ndio na 18 zilizokataa na kulipeleka suala hilo katika baraza la wawakilishi ambalo linadhibitiwa na chama cha Republican , ambalo nalo liliidhinisha hatua hiyo usiku wa jana Jumatano kwa kura 285 dhidi ya 144.

Spika wa baraza la wawakilishi kutoka chama cha Republican John BoehnerPicha: Reuters

Rais barack Obama alitia saini makubaliano hayo ambayo yamefuata masharti yale yale aliyoyatoa wakati matatizo hayo mawili yalipojitokeza zaidi ya wiki tatu zilizopita , muda mfupi baada ya usiku wa manane leo Alhamis. Bunge la Marekani lilikuwa linakabiliwa na muda wa mwisho hadi saa tano na dakika 59 usiku wa jana kuingia leo Alhamis kupandisha mamlaka ya serikali kuweza kukopa ama waliingize taifa hilo katika hatari ya kushindwa kutekeleza majukumu yake.

Mswada huo sasa unaifungua serikali hadi tarehe 15 mwezi Januari mwakani na unaruhusu wizara ya fedha kukopa hadi Februari 7 mwaka ujao ama huenda kwa muda wa mwezi mmoja zaidi.

Hatua hiyo haijumuishi chochote ambacho wabunge wa chama cha Republican walikidai wakitaka kufutwa ama kupunguzwa kwa mpango wa rais Obama wa kufanyia mageuzi mpango wake wa bima ya afya.

Rais Barack ObamaPicha: Reuters

Spika wa baraza la wawakilishi la Marekani John Boehner amesema , "Tumepambana , lakini hatukushinda."

Marekani imekwisha wahi kuwa katika hali kama hiyo hapo kabla, ikisubiri kupata muafaka kuhusu suala la bajeti bila ya kuwa na matokeo ya uhakika. Lakini hii ilikuwa mara ya kwanza katika miaka 17 kwa serikali ya Marekani kufunga baadhi ya shughuli zake muhimu . Kiongozi wa wabunge wa chama cha Democratic katika baraza la wawakilishi Nancy Pelosi aliita hatua hiyo kuwa ni siku 16 za hatari ya kifahari ambayo imeugharimu uchumi wa Marekani karibu dola bilioni 24.

Spika wa baraza la seneti la Marekani Harry Reid wa chama cha Democratic amesema kuwa hiyo ni hatua muhimu kwa Marekani.

"Tumeona leo jinsi bunge lilivyofikia makubaliano ya kihistoria kwa vyama vyote, ili kuiwezesha serikali kufanya kazi zake tena na kuwezesha kulipa madeni yake."

Wafanyakazi wa serikali ya Marekani wakiandamanaPicha: Reuters

Mkwamo huo wa kibajeti ulitikisa masoko duniani na kutishia kuharibu hadhi ya deni la Marekani kama sehemu ambayo haileti hali ya wasi wasi kwa serikali na wawekezaji kuhifadhi fedha zao kwa matrilioni katika fedha za kigeni. Wachache waliitarajia Marekani kushindwa kulipa madeni yake lakini baadhi ya wawekezaji waliuza dhamana za serikali kwa kuhofu juu ya uwezekano wa kucheleweshewa malipo na kuacha kununua hisa ambazo zinaweza kuguswa na mporomoko wa uchumi nchini Marekani.

Mkurugenzi mkuu wa shirika la fedha la kimataifa IMF Christine Lagarde ameyakaribisha makubaliano hayo lakini amesema uchumi wa Marekani unaoyumba yumba unahitaji uimara wa muda mrefu wa bajeti yake.

China na Japan ambazo kila moja inamiliki kiasi cha dola trilioni moja katika hazina ya Marekani, ziliitolea mwito nchi hiyo hapo kabla kufikia makubaliano haraka.

Mwandishi: Sekione Kitojo / ape / dpae / afpe

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW