Bush akamilisha ziara yake ya mashariki ya kati
17 Januari 2008CAIRO:
Rais George W.Bush amekamilisha ziara yake ya siku nane katika eneo la Mashariki ya kati kwa ziara fupi nchini Misri.
Mkutano wake na rais Hosni Mubarak wa Misri, uligubikwa na mgogoro wa Isreal na Palestina. Akizungumza katika hoteli ya Sharm el-Sheikh, rais Bush ameishukuru Misri kwa kuunga mkono mchakato wa amani na kuwa na matumaini kuwa suluhisho litapatikana.Aidha Bush ametoa matumaini kuwa Misri itapiga hatua u mbele zaidi kuelekea demokrasia kamili.Kipindi kilichopita Marekani imekuwa ikiikosoa Misri kuhusu suala la haki za binadamu na jinsi inavyoandama vyombo vya habari vinavyojitegemea. Pia Bush amesema kuwa Syria na Iran ni lazima zikomeshe kuingilia siasa za Lebanon na kuziomba nchi zingine katika kanda hiyo kumuunga mkono Waziri Mkuu Fouad Siniora wa Lebanon.