1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bush azuru Bahrain.

13 Januari 2008

Bahrain. Rais wa Marekani George W. Bush yuko nchini Bahran, ikiwa ni kituo cha tatu katika ziara yake ya siku nane katika mashariki ya kati. Bush ni rais wa kwanza wa Marekani kuizuru Bahrain, ambayo ni makao makuu ya kikosi cha 5 cha jeshi la majini la Marekani. Bush amewasili Bahrain akitokea Kuwait, ambako alipewa maelezo na kamanda wa ngazi ya juu wa jeshi la Marekani jenerali David Petraeus. Bush pia amevitembelea vikosi vya majeshi ya Marekani vilivyoko Kuwait na katika hotuba yake amesema kuwa hatua kubwa zimepigwa nchini Iraq. Amesema kuwa upunguzaji zaidi wa majeshi hayo utaamuliwa kwa msingi wa maelekezo ya majenerali wa Marekani nchini Iraq.

Kuihusu Iran Bush ameitaka nchi hiyo kutoingilia masuala ya Iraq kwa kuwasaidia wanamgambo wanaopigana dhidi ya jeshi la Marekani na jeshi la Iraq.

Iran inapaswa kuacha mara moja kuwaunga mkono makundi maalum ya wanamgambo ambao wanashambulia majeshi ya Iraq na yale ya ushirika wa kimataifa na kuwateka nyara na kuwauwa maafisa wa Iraq.

Rais Bush anatarajiwa kwenda umoja wa falme za Kiarabu UAE na Saudi Arabia kabla ya kituo chake cha mwisho nchini Misr siku ya Jumatano.