1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bwawa kubwa la utata la Ethiopia

Iddi Ssessanga
8 Julai 2021

Ujenzi wa Ethiopia wa bwawa kubwa kwenye Mto Nile, ambao Baraza la Usalama la UN linaujadli Alhamisi, unaongeza mivutano ya kikanda haswa na Misri, ambayo inategemea Mto Nile kwa asilimia 97 ya usambazaji wake wa maji.

Äthiopien Luftbild Grand-Ethiopian-Renaissance-Talsperre
Picha: DW/Negassa Desalegen

Ukiwa na urefu wa kilomita 6,695 (maili 4,160), Mto Nile ni moja wapo ya mito mirefu zaidi ulimwenguni na mtoaji muhimu wa maji na umeme wa maji katika eneo lenye ukame.

Bonde lake la mifereji ya maji ya zaidi ya kilomita za mraba milioni tatu (maili za mraba 1.16 milioni) linapita katika nchi 10: Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Misri, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Sudan Kusini, Sudan, Tanzania na Uganda.

Mito miwili kuu - White Nile na Blue Nile - hukusanyika Khartoum kabla ya kupita kaskazini kupitia Misri na kuingia Bahari ya Mediterania. Karibu mita za ujazo bilioni 84 za maji zinakadiriwa kutiririka kando ya Mto Nile kila mwaka.

Ethiopia mnamo 2011 ilizindua ujenzi wa bwawa la Grand Ethiopia la Renaissance kwenye Blue Nile, takriban kilomita 30 kutoka mpaka na Sudan.

Soma pia: Misri yapeleka mzozo wake na Ethiopia baraza la Usalama

Bwawa hilo lenye thamani ya dola bilioni 4.2 litazalisha megawati zaidi ya 5,000 za umeme, na kulifanya kuwa bwawa kubwa zaidi la umeme barani Afrika na kuongeza maradufu uzalishaji wa umeme wa Ethiopia.

Picha ya Satelait ya bwawa la Grand Ethiopia Renaissance Dam (GERD), ambalo limekuwa chanzo cha mzozo kati ya Ethiopia, Misri na Sudan.Picha: AFP/Maxar Tech

Ethiopia ilianza awamu ya kwanza ya kujaza hifadhi ya bwawa la futi 475 (mita 145) katikati ya mwaka 2020.

Haki ya turufu ya Misri

Misri, taifa kame la karibu watu milioni 100, hutegemea Mto Nile kwa mahitaji yake mengi ya maji, pamoja na kilimo. Cairo inadai haki ya kihistoria ya mto huo kutokana na mkataba wa 1929 kati ya Misri na Sudan uliowakilishwa na mkoloni Uingereza, ambayo iliipa kura ya turufu ya Misri juu ya miradi ya ujenzi kando ya mto huo.     

Mkataba wa 1959 uliongeza mgao wa Misri kwa hadi karibu asilimia 66 ya mtiririko wa maji ya mto huo, na asilimia 22 kwa Sudan. Ethiopia haikuhusika na mikataba hiyo na haiichukulii kuwa halali.

Mnamo mwaka wa 2010 nchi za bonde la Mto Nile, ukiondoa Misri na Sudan, zilitia saini makubaliano mengine, Mkataba wa Mfumo wa Ushirikiano, ambao unaruhusu miradi kwenye mto bila makubaliano ya Cairo.     

Ethiopia, moja ya nchi zenye chumi unaokua kwa kasi barani Afrika katika miaka ya hivi karibuni, inasisitiza kuwa bwawa halitaathiri mtiririko wa maji unaoendelea.

Waziri mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed akiwa katika mkutano na rais wa Misri Abdel-Fattah al-Sisi mwaka 2018.Picha: Imago Images/Xinhua

Hatari kubwa?

Lakini Misri inahofia kuwa ugavi wake utapungua katika muda itachukua kujaza hifadhi yenye uwezo wa mita za ujazo bilioni 74. Misri inaliona bwawa la Ethiopia kama tishio kwa uwepo wake na Sudan imeonya mamilioni ya maisha yatakuwa katika "hatari kubwa" ikiwa Ethiopia itajaza bwawa hilo.

Muongo mmoja wa mazungumzo umeshindwa kuzaa makubaliano. Mapema wiki hii, Misri na Sudan zilisema Ethiopia imeanza awamu ya pili ya kujaza hifadhi, operesheni ambayo bado haijathibitishwa na Addis Ababa. Mkutano wa Baraza la Usalama Alhamisi uliombwa na Tunisia kwa niaba ya Misri na Sudan.

Chanzo kingine cha mvutano wa kikanda ni mzozowa tangu Novemba, katika mkoa wa kaskazini mwaEthiopia wa Tigray, ambao umepelekea wakimbizi wapatao 60,000 kukimbilia Sudan, taifa linalopambana na changamoto zake za kiuchumi.

Majeshi ya Sudan na Ethiopia hivi karibuni yemerejesha shughuli zake katika ukanda wenye rutuba wa mpakani wa Fashaga ambapo wakulima wa Ethiopia wamelima kwa muda mrefu katika ardhi inayodaiwa na Sudan.