CALIFORNIA:idadi ya waliokufa kufuatia moto mkubwa imeongezeka
26 Oktoba 2007Matangazo
Idadi ya watu waliokufa kufuatia mkasa wa moto mkubwa katika jimbo la California nchini Marekani imefikia watu 12 baada ya kupatikana miili ya watu wanne zaidi katika eneo la mlimani karibu na mpaka wa Mexico.
Wazima moto wamejitahidi kuudhibiti moto huo hasa baada hali ya kuvuma upepo kutulia.
Moto mkubwa hata hivyo unaendelea kuwaka katika wilaya ya Orange ambako utawala unashuku kuwa huwenda umeanzishwa makusudi.
Rais George Bush ambae alilaumiwa vikali wakati wa mkasa wa kimbunga cha Katrina ametembelea jimbo la California kujionea hasara iliyosababishwa na moto huo mkubwa, amesema ni muhimu kwake kufika eneo hilo na kujionea hali halisi ilivyo.
Rais Bush alikuwa pamoja na gavana wa jimbo wa California Arnold Schwarzeneger.