Volke Finke atimuliwa kama kocha wa Cameroon
31 Oktoba 2015Matangazo
Uamuzi huo ulifanywa na kamati kuu tendaji ya Shirikisho la Kandanda la Cameroon (Fecafoot) siku ya Ijumaa.
Finke, mwenye umri wa miaka 67, amekuwa akiyanoa makali ya timu hiyo tangu Mei 2013 lakini chini ya uongozi wake, timu hiyo imeandikisha msururu wa matokeo mabaya hasa katika fainali za Kombe la Dunia 2014 na fainali za Kombe la Taifa Bingwa Afrika 2015.
Fecafoot imetangaza kuwa Alexandre Belinga ameteuliwa kama kaimu kocha mkuu wa timu na atasaidiwa na Djonkep Bonaventure.
Makocha hao wawili sasa huenda wakawa ndio watakaoiandaa Cameroon kwa mechi mbili za kufuzu katika Kombe la Dunia 2018 dhidi ya Niger mnamo Novemba 13 na 17.
Mwandishi: Bruce Amani/DPA
Mhariri: Mohamed Dahman