1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Confederations Cup: Nani mbabe leo Brazil na Hispania?

30 Juni 2013

Brazil na Uhispania zinakutana leo jioni(30.06.2013) katika fainali ya kukata na shoka ya kombe la FIFA la mabara, Confederations Cup katika uwanja maarufu mjini Rio de Janeiro wa Maracana.

A general view of Maracana stadium during a media tour ahead the upcoming Confederations Cup in Rio de Janeiro June 7, 2013. REUTERS/Ricardo Moraes (BRAZIL - Tags: SPORT SOCCER)
Uwanja wa Maracana mjini RioPicha: Reuters

Wenyeji Brazil wanasisitiza kuwa wanaweza kuwanyima mabingwa hao wa dunia na bara la Ulaya Uhispania fursa adimu ya kudhibiti mataji yote makuu duniani kwa wakati mmoja.

"Uhispania inang'ara, lakini kama timu nyingine ina mapungufu yake," amesisitiza kocha wa Brazil Luiz Felipe Scolari jana Jumamosi.

"Siiangalii Uhispania kama wenye uwezo wa kutwaa taji hili."

Maandamano yanaendelea

Watayarishaji na washiriki wanatarajia tukio la fainali hiyo kutoingia doa kutokana na ghasia za kijamii ambazo zimeonekana katika wakati wote wa mashindano hayo.

Waandamanaji wakiandamana mjini RioPicha: Christophe Simon/AFP/Getty Images

Maandamano ambayo kimsingi yalikuwa yakipinga kupanda mno kwa nauli za usafiri wa mjini yaliingia katika sura ya upinzani wa umma dhidi ya kile wanaharakati walichosema kuwa ni uongozi mbovu wa serikali pamoja na huduma mbovu za kijamii.

Katika muktadha huo , waandamanaji wanasema , fedha nyingi zilizotumika katika kuandaa matukio ya kimichezo hayakubaliki. Zaidi ya wananchi milioni 1.5 wa taifa hilo wenyeji wa mashindano ya Confederations Cup pamoja na kombe la dunia mwakani waliingia mitaani kupinga na wanaharakati wameitisha maandamano mapya leo Jumapili.

Mara hii ni ya tisa kukutana

Katika dimba lenyewe, timu zilizofanikiwa kuingia katika fainali zimekutana kwa mara nane hapo kabla. Brazil ilishinda mara nne na Uhispania imeshinda mara mbili na michezo miwili ilikuwa sare.

Kikosi cha UhispaniaPicha: Reuters

Pambano la hivi karibuni kabisa lilikuwa mwaka 1999 katika mchezo wa kirafiki.

Iwapo historia itakuwa upande wa Waamerika ya kusini, lakini Uhispania haijapoteza mchezo wowote wa mashindano katika michezo 29 iliyoshiriki, tangu iliposhindwa na Uswisi mwanzoni mwa fainali za kombe la dunia mwaka 2010 nchini Afrika kusini.

Tangu iliposhinda fainali za kombe la mataifa ya Ulaya Euro 2008, na kujivua nuksi ya kukosa mataji tangu mwaka 1964, Uhispania imejikusanyia kila taji lililokuwa mbele yao.

Ushindi wao mwaka 2008 umekuja chini ya kocha Luis Aragones, lakini mrithi wake Vicente del Bosque ameweza kukifanya kikosi hicho kucheza na kufikia hali ya kuonekana kinaweza kila kitu.

Kocha wa Uhispania Vicente del BosquePicha: AP

Ushindi wa Uhispania wa kombe la dunia mwaka 2010 na kombe la mataifa ya Ulaya "Euro 2012" umekifanya kikosi hicho kuwa timu ya kwanza ya taifa kunyakua mataji matatu makuu ya kimataifa.

Brazil yaazimia kurejesha hadhi yake

Katika miaka ambayo Brazil ilikuwa imekusanya jumla ya mataji matano ya kombe la dunia kuanzia mwaka 1958, kikosi cha Uhispania licha ya kunyakua kombe la Ulaya mwaka 1964, kilikuwa kimetumbukia katika adha ya nuksi ya kukosa mataji.

Kocha wa Brazil Luiz Felipe ScolariPicha: EVARISTO SA/AFP/Getty Images

Mara ya mwisho timu hizo kukutana katika mchezo ambapo zilikuwa zinawania tuzo ilikuwa katika awamu za mwanzo za kombe la dunia mwaka 1986. Brazil ilishinda kwa goli moja katika mchezo ambao Uhispania ilifanikiwa kuuweka mpira wavuni mara fulani lakini juhudi zao hizo zilikataliwa na refa.

Scolari anaona dalili njema katika siku ya tarehe ya mchezo wenyewe leo Jumapili, Juni 30 ambapo ni tarehe ambayo kikosi chake cha zamani cha Brazil kilishinda kombe la dunia mwaka 2002.

Italia na Uruguay pia zinakipiga leo kutafuta mshindi wa tatu katika mashindano hayo.

Mwandishi : Sekione Kitojo / afpe

Mhariri: Mohammed Khelef

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW