Costa aitaka Iran kusitisha mashambulizi Mashariki ya Kati
31 Machi 2026
Baada ya mazungumzo ya simu na Masoud Pezeshkian, Antonio Costa amesema amesisitiza haja ya kupunguza makali ya mapigano, kulinda raia na miundombinu ya kiraia, pamoja na pande zote kuheshimu sheria za kimataifa.
Ameitaka Iran kusitisha mashambulizi aliyoyaita yasiyokubalika dhidi ya mataifa ya kanda na kujihusisha kikamilifu katika juhudi za kidiplomasia.
Costa ameongeza kuwa hatua hiyo pia inahusisha kushirikiana na Umoja wa Mataifa ili kuhakikisha uhuru wa usafirishaji katika Mlango-Bahari wa Hormuz, akisisitiza kuwa lazima kuwe na nafasi ya diplomasia.
Hegseth asema uwezo wa Iran unapungua
Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth amesema mashambulizi ya Marekani yanaendelea kuipa Marekani nguvu zaidi katika uwanja wa vita huku uwezo wa Iran ukipungua.
"Hii ni kuhusu urithi. Mafanikio ni muhimu. Na kwa sababu ya rais huyu na Wamarekani hawa, tunakaribia ushindi zaidi kuliko hapo awali. Rais Trump anafanya kile ambacho hakuna rais mwingine aliyekuwa na ujasiri wa kukifanya. Marais waliopita walikuwa wa maneno, lakini yeye ni wa vitendo. Katika uwanja wa vita, kutokana na uhuru aliotupa, nguvu ya mashambulizi ya Marekani inaongezeka. Sisi tuna chaguo nyingi zaidi, wao wana chache.”
Trump azitaka nchi zilizojitenga na vita Iran kujitegemea
Rais Donald Trump amezitaka nchi ambazo hazikushiriki katika mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran kununua mafuta kutoka Marekani au kwenda katika Mlango-Bahari wa Hormuz na "kuyachukua.”
Kupitia mtandao wake wa Truth Social, Trump aliitaja Uingereza kuwa miongoni mwa nchi ambazo hazikushiriki, akizitaka kujitegemea na kuongeza kuwa Marekani haitakuwa tayari tena kusaidia kama ilivyokuwa awali.
Qatar yasema mataifa ya Ghuba yana msimamo mmoja
Qatar imesema mataifa ya Ghuba yana msimamo mmoja wa kutaka kupunguzwa kwa mapigano na kumalizika kwa vita vya Mashariki ya Kati, wakati Iran ikiendelea na mashambulizi mapya dhidi ya majirani zake.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Qatar, Majed al-Ansari, amesema kuna umoja mkubwa katika kanda hiyo wa kuhimiza kupungua kwa mvutano na kusitishwa kwa vita.
Saudi Arabia yaokoa meli ya mafuta ya Kuwait
Mamlaka nchini Saudi Arabia zimesema meli ya mafuta ya Kuwait iliyoshambuliwa imeokolewa salama bila kuripotiwa kwa majeruhi wala uvujaji wa mafuta. Mapema, ofisi ya habari ya Dubai ilisema droni ililenga meli hiyo katika eneo la maji la Dubai.