1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Janga

Covid yazidisha ukosefu wa usawa kati ya wanaume na wanawake

Ibrahim Swaibu
1 Septemba 2020

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametahadharisha kwamba janga la COVID-19 limeongeza kukosekana kwa usawa wa kijinsia pamoja na kuendelea kuzorota kwa haki za wanawake.

UN-Generalsekretär Antonio Guterres
Picha: Imago Images/Xinhua/

"Janga la COVID-19 linazidi kutuonyesha tu kile ambacho sote tunaelewa, miaka mingi ya dunia kutawaliwa na wanaume, utamaduni ambao unaathiri kila mmoja, unaathiri wanawake, wanaume, wasichana na wavulana. Huu ni wakati wa kujenga upya jamii yenye usawa inayomhusisha kila mmoja na yenye ujasiri.”

Hayo aliyasema katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa  Antonio Guterres wakati akizungumza na wanawake wa asasi za kiraia katika mkutano uliofanyika kwa njia ya mtandao siku ya Jumatatu.

Soma zaidi:WHO yautaka ulimwengu kupambana vikali na COVID-19 

Guterres alisema licha ya wanawake kuwa katika mstari wa mbele kupambana dhidi ya COVID 19 wakichangia kati ya 70% na 90% ya wahudumu wa afya, kinachosikitisha ni kwamba ni 30% tu wanawake hao walio katika nafasi zinaowawezesha kuchukua uamuzi.

Picha: webtv.un.org

Aidha kiongozi huyo alielezea wasi wasi wake kuhusu ripoti za mamilioni ya wasichana kutohudhuria shule kutokana na kadhia ya virusi vya Corona pamoja na hofu ya kuongezeka kwa mimba za utotoni. Antonio Gutteres amesema ana wasi wasi juu ya ikiwa wasichana hao wataweza kurejea shuleni.

Soma pia: Mkakati mkali wa Uganda wafanikiwa kudhibiti COVID

Mwito kwa serikali kutoa huduma za afya kwa wanawake

Kadhalika amesema janga la COVID-19 limefichua changamoto wanazopitia wanawake wakitafuta haki zao huku akizitolea wito serikali duniani kuhahikisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wanawake.

"Serikali lazima zitambua kwamba janga hili limesababisha athari kwa huduma za afya. Wanawake wana haki ya kupata huduma bora za afya ya uzazi," alisema katibu mkuu Guterres, na kuongeza kuwani jukumu la serikali kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata huduma hizi hata katika wakati wa janga.

"Tunahitaji mifumo ya afya ambayo inatoa huduma kwa kila mmoja ikiwemo wanawawke na wasichana. Na hii inamaanisha kupaumbele ufadhili kwa huduma msingi ya afya,” alisisitiza katibu mkuu huyo.

Katika mkutano huo, katibu mkuu Guitteres pia aligusia na kuonyesha masikitiko yake kutokana na ripoti za kuongezeka kwa visa vya ukatili dhidi ya wanawake, hasa katika kipindi hiki cha virusi vya Corona ambapo wanawake wengi wanalazimika kushinda nyumbani na wale aliowaiita wanyanyasaji wao.

Soma zaidi: Afrika: Visa vya COVID-19 vyapindukia milioni moja

Aidha, ametahadharisha kuwa iwapo hakutokuwepo jitihada za haraka, huenda ikarejesha nyuma hatua ziliopigwa katika usawa wa kijinsia pamoja na kuzidisha visa vya ukiukaji wa haki za wanawake.

Wakati huo huo, Umoja wa Mataifa umezitolea wito serikali duniani, kuyapa kupaumbele masuala ya kulinda haki za wanawake hasa katika mipango yao ya kitaifa ya kupambana dhidi ya COVID-9 ikiwemo kukomesha ukatili dhidi ya wanawake.

Chanzo. APE

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW