1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Daktari wa zamani wa Rwanda apandishwa mahakamani Paris

1 Oktoba 2024

Eugene Rwamucyo, aliyekuwa daktari nchini Ufaransa na Ubelgiji baada ya kukimbia kutoka Rwanda, anafikishwa mahakamani mjini Paris, Ufaransa, kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya kimbari ya Rwanda miongo mitatu iliyopita.

Kigali, Rwanda, Paul Kagame, mauaji ya Kimbari ya 1994
Rais Paul Kagame wa Rwanda akizungumza kwenye Kumbukumbu ya Miaka 30 ya Mauaji ya Kimbari ya 1994.Picha: Jean Bizimana/REUTERS

Rwamucyo, mwenye umri wa miaka 65, anatuhumiwa kuhusika kuzisaidia mamlaka za nchi yake katika kuendeleza propaganda dhidi ya jamii ya Watutsi pamoja na kushiriki kwenye mauaji ya watu wengi katika juhudi za kuharibu ushahidi wa mauaji ya kimbari.

Daktari huyo wa zamani anashtakiwa kwa mauaji, kushirikiana na wauwaji, uhalifu dhidi ya ubinaadamu, kushiriki kwenye uhalifu dhidi ya ubinaadamu pamoja na kula njama ya kuandaa matukio hayo ya uhalifu.

Soma zaidi: Rwanda: Kumbukumbu ya miaka 27 tangu kutokea mauaji ya kimbari

Endapo atakutwa na hatia, huenda akakabiliwa na kifungo cha maisha jela.  

Wakili wake, Philippe Meilhac, amesema mteja wake amekanusha kuhusika na makosa ya aina yoyote na kwamba tuhuma zinazomuandama zinatokana na hatua yake ya kuipinga serikali ya sasa nchini Rwanda.

Takribani mashahidi 60 wanatarajiwa kutoa ushahidi mbele ya mahakama katika kesi hiyo itakayoendelea hadi Oktoba 29.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW