1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Erdogan aonya hatari ya mashambulizi Idlib

Isaac Gamba
5 Septemba 2018

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan ameonya kuwa mashambulizi ya makombora na mabomu katika mkoa wa  mwisho unaloshikiliwa na waasi  wa Idlib nchini Syria  yanaweza kusababisha maafa makubwa.

Türkei 1. Jahrestag nach Putschversuch Präsident Erdogan
Picha: Reuters/U. Bektas

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan ameonya kuwa mashambulizi ya makombora na mabomu katika mkoa wa  mwisho unaloshikiliwa na waasi  wa Idlib nchini Syria  yanaweza kusababisha maafa makubwa .  Isaac Gamba anaraarifu zaidi katika taarifa ifuatayo.

Kwa mujibu wa gazeti la kila siku nchini Uturuki la Hurriyet, Erdogan amewaeleza waandishi wa habari  mara baada ya kumalizika ziara yake katika jimbo la Kyrgystan  barani Asia   kuwa kutakuwa na mauaji makubwa  kama mashambulizi ya makombora yataendelea  mjini Idlib.

Matamshi hayo ya Erdogan yanakuja mnamo wakati vikosi vya Syria vikizidi kujikusanya  jirani na jimbo la magharibi la Idlib kwa lengo la kufanya shambulizi kubwa  ambalo tayari limeibua hofu kubwa tangu mgogoro huo ulipoanza miaka saba iliyopita.

Syria  na mshirika wake mkuu Urusi  wameapa  kuyaondoa kabisa yale wanayoyaita makundi ya itikadi kali  yanayodhibiti kwa sasa jimbo la Idlib.

Ama kwa upande wake Mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini Syria Stafafan De Mistura amesema jitihada za kujaribu kuzia mapigano katika jibo la Idlib zinaendelea.

Hayo yanajiri wakati Urusi mshirika wa karibu wa rais Bashar Assad  jana Jumanne  ikianzisha tena mashambulizi ya anga  katika jimbo la Idlib ikiwa ni baada ya kusimamisha mashambulizi hayo kwa siku 22.

Uturuki ambayo inawaunga mkono baadhi ya wapiganaji wa makundi ya waasi  imekuwa ikifanya mazungumzo mara kadhaa na Urusi pamoja na Marekani  yanayolenga  kuzuia mashambulizi katika jimbo la Idlib.

 

Watu watatu wauawa Syria

Baadhi ya wapiganaji wa makundi ya waasi nchini SyriaPicha: Getty Images/AFP/O.H. Kadour

Wakati huohuo  kiasi ya watu watatu  wameuawa na wengine 23 kujeruhiwa katika shambulizi la anga linaloshukiwa kufanywa na ndege za Israel katika maeneo ya yanayodhibitiwa na serikali ya Syria  pamoja na vikosi vya Iran nchini humo.

Shirika la waangalizi wa haki za binadamu nchini Syria lenye makao yake nchini Uingereza limesema mashambulizi hayo yamefanyika  katika jimbo la magharibi la Hama na katika mji wa Banias.

Shirika hilo limesema wengi wa waliojeruhiwa walikuwa ni wanajeshi wa Syria na kuwa idadi ya vifo inaweza kuongezeka kutokana na hali mbaya walionayo baadhi ya majeruhi.

Vyombo vya habari vya serikali ya Syria   vimeripoti jana Jumanne kuwa  mfumo wa nchi hiyo wa kujikinga dhidi ya makombora ulizuia  mashambulizi ya maroketi ya Israel.

Chanzo cha habari kutoka makundi ya waasi kinasema mashambulizi hayo ya Israel yalilenga ghala la silaha  la vikosi vya serikali ya Syria pamoja na washirika wake Iran.

Hata hivyo hakukuwa na taarifa  rasmi kutoka Israel kuthibitisha mashambulizi hayo.

Wakati hayo yakiendelea marais wa Iran, Urusi na Uturuki wanakutana Ijumaa wiki hii mjini Tehran kawa ajili ya mkutano wa kilele kujali mstakali wa jimbo la Idlib nchini Syria.

Urusi na mshirika wake  mkuu Urusi  wameapa  kuyaondoa kabisa makundi ya waasi yanayodhibiti kwa sasa jimbo la Idlib  lakini mkutano huo wa Ijumaa huenda ukaamua  ni jinsi gani mashambulizi kwenye jimbo hilo yatafanyika.

Mwandishi: Isaac Gamba/AFPE/DPAE

Mhariri : Mohammed Abdul-Rahman

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW