1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Erdogan asema mradi wa ujenzi utaendelea bustani ya Taksim

6 Juni 2013

Polisi wa Uturuki wamepambana na waandamanaji jana kabla ya waziri mkuu Tayyip Erdogan kurejea nchini humo akitokea katika ziara ya mataifa ya Afrika kaskazini. Waziri mkuu Erdogan anarejea leo Alhamis(06.06.2013)

epa03730563 Activists perform yoga at the Gezi Park in Istanbul, Turkey 04 June 2013. More than 2,300 people have been injured and one person killed during four days of fierce clashes between protesters and police in Turkey, according to a doctors' association, as the prime minister blamed 'extremist elements' for the riots. More than 1,480 people have been wounded in clashes in Istanbul, the country's largest city, with some 800 more injured in the capital Ankara and the Aegean city of Izmir. EPA/TOLGA BOZOGLU
Watu wakifanya mazoezi ya Yoga katika bustani ya Gezi mjini IstanbulPicha: picture-alliance/dpa

Waziri mkuu Recep Tayyip Erdogan amesema leo kuwa serikali yake itaendelea na mpango wake wenye utata wa kuibadilisha bustani ndogo katikati ya jiji la Istanbul , licha ya maandamano makubwa dhidi ya ujenzi unaotarajiwa kufanywa katika uwanja huo maarufu wa Taksim.

Akizungumza na waandishi habari mjini Tunis baada ya kukutana na mwenzake wa Tunisia , Erdogan amesema makundi yanayotuhumiwa kuhusika na ghasia zilizofanyika hapo kabla yanatumia kile kilichoanza kama maandamano ya walinzi wa mazingira na kwamba idadi kubwa ya watu kutoka mataifa ya nje wamekamatwa.

Waandamanaji mjini IstanbulPicha: Reuters

Erdogan anarejea

Erdogan atawasili nyumbani leo akitokea katika ziara ya mataifa ya Afrika ya kaskazini na kukabili madai ambayo aliomba radhi kwa ajili ya matumzi makubwa ya nguvu ya polisi katika siku sita za maandamano, ambapo watu watatu wameuwawa na zaidi ya watu 4,000 wamejeruhiwa katika miji kadha, na kuwafuta kazi wale walioamuru kitendo hicho.

Watu walioshuhudia wamesema kuwa polisi wa kuzuwia ghasia walifyatua mabomu ya kutoa machozi dhidi ya mamia ya waandamanaji ambao walikuwa wakiwarushia mawe na kuimba nyimbo za kumpinga Erdogan katikati ya mji mkuu Ankara jana usiku.

Polisi wakipambana na waandamanaji mjini IstanbulPicha: Reuters

Katika jimbo la mashariki la Tunceli , mamia ya waandamanaji waliweka vizuwizi vya vyuma na pia waliwarushia mawe polisi , ambao nao walijibu kwa kufyatua mabomu ya kutoa machozi. Istanbul , mji ambao umeshuhudia mapambano makali , ulikuwa shwari usiku wa jana.

Waandamanaji hawataki uwanja kujengwa

Kile kilichoanza kama kampeni dhidi ya ujenzi katika bustani yenye miti mingi mjini Istanbul iligeuka kuwa mapambano makubwa na upinzani mkubwa kwa kile kinachoonekana kuwa ni utawala wa kimabavu wa Erdogan na chama chake cha kinachofuata nadharia za dini ya Kiislamu cha AK.

Polisi walisaidiwa na magari ya deraya wamepambana na waandamanaji usiku baada ya usiku, wakati maelfu ya watu walijikusanya kwa amani katika siku za hivi karibuni katika uwanja wa Taksim, ambako maandamano yalianzia.

Polisi ambaye alianguka kutoka katika daraja wakati akiwafukuza waandamanaji katika mji wa kusini wa Adana amefariki kutokana na majeraha aliyoyapata, imeeleza televisheni ya Uturuki, ikiwa ni kifo cha tatu kinachohusishwa na maandamano hayo.

Waziri mkuu mbishi

Waziri mkuu Erdogan aliondoka siku ya Jumatatu akiwa katika hali ya kukaidi, akiwapuuzia waandamanaji kuwa ni waporaji na kusema ghasia hizo zitamalizika katika muda wa siku chache, matamshi ambayo wakosoaji wake wamesema wamechochea zaidi hali ya mvutano.

Waziri mkuuRecep Tayyip Erdogan akiwa mjini TunisPicha: Reuters

Waziri mkuu Erdogan ameongeza leo(06.06.2013) kuwa wanachama wa kundi la kigaidi wameshiriki katika maandamano ya kuipinga serikali yanayoikumba nchi hiyo. Amesema kuwa watuhumiwa saba kutoka nje ya nchi hiyo wanaohusishwa na machafuko hayo wamekamatwa. Miongoni mwa waandamanaji, kuna watu wenye msimamo mkali, baadhi yao wakihusishwa na ugaidi, Erdogan amewaambia waandishi habari katika siku yake ya mwisho ya ziara ya mataifa ya Afrika ambayo imegubikwa na hali ya machafuko nchini mwake.

Wakati huo huo kamishna wa haki za binadamu nchini Ujerumani leo ameyaeleza matumizi ya nguvu dhidi ya waandamanaji nchini Uturuki kuwa yakustusha, na kuitaka serikali kuwaacha huru mara moja watu waliowekwa kizuwizini, ambao amesema wanapigania haki zao za msingi.

Markus Leoning kamishna wa haki za binadamu wa serikali ya Ujerumani amesema katika taarifa kuwa anaitarajia serikali ya Uturuki kujibu maandamano ya amani kwa njia bora na sio kutumia nguvu.

Mwandishi : Sekione Kitojo / afpe / rtre

Mhariri: Mohamed Khelef

Ruka sehemu inayofuata Gundua zaidi
Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW