1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ethiopia iko tayari kupeleka majeshi yake Somalia kusaidia kikosi cha AMISOM

Josephat Nyiro Charo12 Agosti 2010

Ethiopia imesema itakuwa tayari kuyarudisha majeshi yake nchini Somalia kuyasaidia majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Afrika. Wakati huo huo, vikosi vya usalama huko Puntland vimefaulu kuidhibiti kambi ya wanamgambo

Wanajeshi wa serikali ya Somalia wakipiga doria mjini MogadishuPicha: AP

Waziri mkuu wa Ethiopia Meles Zenawi,amewaeleza waandishi habari jijini Addis Ababa,kuwa kuwa nchi yake ipo tayari kupeleka majeshi yake nchini Somalia iwapo itatakiwa kufanya hivyo na kitengo maalumu cha Umoja wa Afrika,kinachoisaidia serikali ya Somalia,AMISOM.

Zenawi ameeleza kuwa nchi yake itatoa kila aina ya msaada kutoka upande wa pili wa mpaka unaotenganisha nchi hizo,lakini haitovuka mipaka hiyo,iwapo serikali ya mpito ya Mogadishu itaendelea kutishiwa,na kueleza kuwa majeshi yake hayatosita kuvuka mpaka huo,iwapo majeshi ya AMISOM,nayo yatatishiwa na kuhitaji msaada wa Ethiopia,hawatasita kuingilia kati.

Amefafanuwa kwamba kuingilia kati kwa Ethiopia,kutatilia mkazo zaidi katika kuyasaidia majeshi ya AMISOM,kwa kuwarahisishia kuvuka mpaka na kuingia Ethiopia,na kueleza kuwa majeshi yake yapo tayari kuingia na kuvuka mpaka wa Somalia,licha ya kueleza kuwa uwezekano huo unaweza kuwa mdogo kutokea.

Viongozi wa Afrika,walikubaliana mwezi uliopita kulisaidia zaidi jeshi la AMISOM,kufuatia mashambulizi ya mabomu jijini Kampala,na kusababisha vifo vya raia wapatao 80 mwezi Julai mwaka huu,ambapo kundi la Al Shabaab lilikiri kuhusika na shambulio hilo.

Kundi hilo la uasi la Al Shabaab,lilieleza kuwa shambulizi hilo,linatokana na Uganda kupeleka majeshi yake nchini Somalia,kwa nia ya kuongeza nguvu jitihada za kulinda amani,ambapo maelfu ya watu wamekuwa wakiuawa na wengine kuyakimbia makazi yao jijini Mogadishu,eneo ambalo linatajwa kuwa ni hatari zaidi duniani,linalokabiliwa pia na maafa ya matatizo ya haki za binaadamu.

Wakati huo huo,majeshi ya kulinda amani nchini Somalia,wametangaza kulidhibiti eneo la Puntland,ambalo lilikuwa likitumiwa kama kambi ya kijeshi na mtandao wa Al Qaeda,lililokuwa chini ya himaya ya kiongozi wa mtandao huo,Mohamed Said Atom.

Majeshi ya Puntland,yalianzisha mashambulizi siku ya Jumapili,ikiwa ni wiki 2 baada ya kushambuliwa na vikundi vya wapiganaji vilivyo chini ya Atom,ambaye ni miongoni mwa watu wanaosakwa na Umoja wa mataifa,kwa kipindi kirefu.

Kiongozi wa jeshi la Puntland,Muhammed Abdilrahman ameliambia shirika la habari la AFP kuwa kulitokea ufyatulianaji wa risasi na vikundi vya uasi katika kijiji cha Galgala,maeneo ya milima yaliyo kaskazini ya Somalia,kabla ya waasi hao kuzidiwa nguvu na kukimbia.

Kiongozi mwingine wa Puntland,eneo lililojitenga na kujitangaza huru kutoka Somalia,Luteni Kanali Omar Abdullahi ameeleza kuwa katika mashambulio hayo,askari 2 wa Puntland waliuawa,ambapo pia walifanikiwa kuwauwa waasi 7,ambao wanapewa mafunzo ya kijeshi na Muhammed Atom.

Kwa upande mwingine,kamanda wa majeshi ya uasi Abdilkarim Ahmed Beynah amekanusha taarifa hizo,na kueleza kuwa majeshi ya Puntland yamekumbana na upinzani mkali kutoka kwa majeshi yao,na kueleza kuwa wamepoteza wanajeshi wengi zaidi kuliko walivyotarajia,na kueleza kuwa wanajeshi wengi watakufa katika vita hivyo.

Mwandishi; Ramadhan Tuwa/AFPE

Mhariri;Josephat Charo

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW