1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

EU, Uingereza zafanya kikao cha dharura

Sylvia Mwehozi
10 Septemba 2020

Maafisa wa ngazi ya juu wa Umoja wa Ulaya wanafanya mazungumzo ya dharura na maafisa wa Uingereza kuhusiana na mpango wa nchi hiyo kukiuka baadhi ya vipengele vya makubaliano ya Uingereza kujitoa katika Umoja wa Ulaya

Symbolbild Brexit Verhandlungen
Picha: picture-alliance/empics/S. Rousseau

Hatua hiyo ya Uingereza ya kuvunja sheria za kimataifa kwa kukiuka baadhi ya vipengele vya makubaliano ya kujiondoa Umoja wa Ulaya, imewashtua viongozi wa muungano huo na inatishia kuyasambaratisha mazungumzo magumu kuhusu mustakabali wa uhusiano wa kibiashara. Soma zaidi: Uingereza na Umoja wa Ulaya zaandaa awamu ya tatu ya mazungumzo ya kibiashara

Afisa mkuu wa Bunge la Ulaya anayehusika na utekelezaji wa makubaliano ya pande hizo mbili Danuta Huebner amesema "hatua kama hiyo ya waziri mkuu Borris Johnson itadhoofisha makubaliano ya kujiondoa na kuharibu imani tuliyonayo kwa washirika wetu wa Uingereza", akiongeza kuwa hilo haliwezi kutokea na halikubaliki.

Uingereza ilikiuka baadhi ya vipengele vya makubalianoPicha: AFP/N. Halle'n

Wiki hii serikali ya kihafidhina ya waziri mkuu Boris Johnson ilitangaza kwamba itaweka sheria itakayojipa mamlaka ya kuvikwepa baadhi ya vipengele vya makubaliano ya Brexit yanayohusisha biashara na eneo la Ireland ya Kaskazini. Hii leo imesisitiza kwamba itajaribu kusukuma muswada ili upitishwe kuwa sheria, ambao umepangwa kujadiliwa katika kikao cha bunge kinachoanza Jumatatu.

Makamu wa Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya, Marcos Sefcovic ameelekea London akitaka "ufafanuzi" na atakutana na waziri wa Uingereza anayehusika na masuala ya Brexit Michael Gove katika mazungumzo yaliyoandaliwa kwa haraka. Sefcovic amesema kuwa anaenda kuelezea wasiwasi mkubwa ilionao Umoja wa Ulaya juu ya muswada uliopendekezwa. Soma zaidi:Umoja wa Ulaya waionya Uingereza kuhusu mktaba wa Brexit

Maafisa hao wawili wanaongoza kamati ya pamoja inayohusika kupanga kanuni za baada ya Brexit kwa ajili ya Ireland ya Kaskazini, sehemu pekee ya Uingereza inayoshirikiana mipaka na Ireland ambayo ni mwanachama wa Umoja wa Ulaya.

Muswada huo utawapatia mawaziri wa Uingereza nguvu za upande mmoja za kudhibiti biashara kati ya England, Scotland, Wales na Ireland ya Kaskazini, pindi tu kipindi cha mpito cha baada ya Brexit kitakapoisha mwishoni mwa mwaka huu.

Lakini chini ya makubaliano ya kujiondoa Umoja wa Ulaya, Uingereza inatakiwa kuwasiliana na Brussels juu ya mipango ya Ireland ya Kaskazini, ambayo itakuwa na mpaka pekee wa ardhi ya Uingereza na Umoja wa Ulaya na ambako miaka 30 ya umwagaji damu ilimalizika na makubaliano ya kihistoria ya amani kufikiwa mnamo mwaka 1998.

Rais wa Baraza la Ulaya Charles Michel anahudhiriaPicha: picture-alliance/AP Photo/F. Seco

Uingereza ilijiondoa kwenye mfumo wa kisiasa wa Umoja wa Ulaya hapo Januari 31. Pande hizo mbili zinajaribu kufikia makubaliano mapya ya kibiashara, lakini mazungumzo yamekwama juu ya masuala kadhaa ikiwemo haki ya uvuvi katika maji ya Uingereza na kanuni za ushindani sawa wa biashara. Soma zaidi: Mpango wa Uingereza wa Brexit waibua wasiwasi Umoja wa Ulaya

Wakosoaji wa Johnson wanasema muswada mpya unalenga kuugeuza mwelekeo ambapo Uingereza itakuwa huru kuunda ushirikiano mpya wa kibiashara bila ya uangalizi wa Umoja wa Ulaya na Marekani. Hata hivyo, spika wa Baraza la wawakilishi la Marekani, Nancy Pelosi alitoa kwa ufupi matumaini yoyote ya Uingereza ya bunge kuidhinisha makubaliano ya baadae ya kibiashara ikiwa itasonga mbele na muswada mpya wa Brexit.

Katika taarifa yake Pelosi amesema Uingereza inapaswa kuheshimu itifaki ya mkataba wa Ireland Kaskazini na Umoja wa Ulaya ambao unazingatia biashara isiyo na mipaka na mwanachama wa Umoja wa Ulaya, Ireland kama njia ya kuheshimu mkataba wa mwaka 1998.

afp, reuters, dpa, ap

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW