1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wito wa mpango wa kufufua uchumi wa Ulaya watolewa

6 Aprili 2020

Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen ametoa mwito wa kuanzishwa mpango wa kufufua uchumi wa mataifa ya Ulaya, huku akihimiza kutengwa fedha kwa ajili ya bajeti ya EU kutokana na janga la corona.

EU Ursula von der Leyen
Picha: Reuters/F. Lenoir

Rais huyo wa halmashauri ya Umoja wa Ulaya amezitaka nchi wanachama wa Umoja huo ziwekeze mabilioni ya fedha ili kuepusha madhara makubwa  katika uchumi yaliyosababishwa na janga la maambukizi ya virusi vya corona.

Bibi Ursula von der Leyen amesema katika makala aliyoandika kwenye gazeti la "Welt am Sonntag" kwamba Umoja wa Ulaya unahitaji mpango maalumu wa kujenga upya uchumi, kama ule ulioanzishwa na Marekani barani Ulaya na kutekelezwa kuanzia mwaka 1948 hadi 1952.

Ameeleza kuwa bajeti ya Umoja wa Ulaya imekubaliwa  na nchi zote wanachama kama njia ya kuondosha  tofauti katika moyo wa mshikamano, na kwamba sasa  fedha hizo zinapaswa kutumiwa kwa ajili ya kukabiliana na mgogoro uliopo.

Ameeleza katika makala hiyo kwamba mabilioni ya fedha zitakazoekezwa ili kuepusha maafa makubwa zitaleta mshikamamo wa marika yote  yafuatayo. Amesema janga la corona linaweza kuwa fursa ya kufufua hisia za mshikamano miongoni mwa  mataifa ya Ulaya.

Hatua za kiuchumi za haraka zinapaswa kuchukuliwa mara moja

Waziri Mkuu wa Uhispania Pedro SanchezPicha: picture-alliance/dpa/Bildfunk/M. Fernandez

Waziri Mkuu wa Uhispania Pedro Sanchez ameunga mkono kuanzishwa kwa mpango huo wa kufufua uchumi, kama ule uliotekelezwa barani Ulaya baada ya kumalizika vita vikuu vya pili. Waziri mkuu wa Uhispania pia amezitaka nchi za Ulaya zichukue hatua za kiuchumi za haraka kana kwamba zimo vitani.

Sanchez amesema barani Ulaya zinahitajika hatua za kiulinzi, ujenzi mpya na mpango wa kuufufua uchumi na kwamba hatua hizo zinapaswa kuchukuliwa mara moja kwa lengo la kuzisaidia nchi zilizoingia katika madeni kutokana na janga la maambukizi ya virusi vya corona.

Bwana Sanchez amesema virusi vya corona  havikuchagua nchi na kwa hivyo mfuko wa fedha utapaswa kuleta manufaa kwa wote na kwamba mgogoro uliopo unaweza kuwa fursa ya ujenzi mpya wa Umoja wa Ulaya wenye nguvu kubwa zaidi.

Umoja huo kwa sasa umetingwa na mjadala juu ya njia za kukabaliana na mzigo wa madeni miongoni mwa nchi wanachama. Mawaziri wa fedha wa jumuiya hiyo wanatarajiwa kukutana hapo kesho Jumanne kujadili juu ya fedha za jumuiya yao wakati huu wa kukabiliana na janga la corona.

Chanzo:/ https://p.dw.com/p/3aTD8

Mhariri: Iddi Ssessanga

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW