Gaddafi atoa ujumbe kwa wafuasi wake
2 Septemba 2011Wakati watawala wapya wa mpito walipokuwa wakikutana na viongozi wengine wa dunia mjini Paris Ufaransa, kujadili ujenzi mpya wa nchi hiyo,kiongozi aliyetimuliwa nchini Libya, Muammar Gaddafi, amezuka na kuwaomba wafuasi wake wajitokeze kutoka mafichoni na waendelee kupigana.
Katika ujumbe uliotangazwa kwenye televisheni ya satelaiti katika kuadhimisha mapinduzi yaliyomuingiza madarakani mnamo mwaka 1969, Gaddafi aliomba mapigano nchini humo yawe ya muda mrefu. Katika matamshi mengine baadaye, Gaddafi aliapa kuzuia usafirishaji wa mafuta katika aina ya tishio linalozusha hofu lenye mfano wa ghasia za nchini Iraq.
Huku kukiwepo taarifa zinazotofautiana kuhusu mahali aliko kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 69, kamanda mmoja kwenye kikosi cha baraza linaloiongoza nchi hiyo, alisema Gaddafi alikimbilia katika mji uliopo jangwani kusini mwa mji mkuu Tripoli.
Vikosi vya upinzani vimerefusha kwa wiki moja muda wa mji alikozaliwa Gaddafi, Sirte, kujisalimisha, katika kutafuta kuzuia umwagikaji damu zaidi.
Mwandishi:Maryam, Abdalla/alle alt VT
Mhariri:Charo, Josephat