1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ghasia nchini Misri Udugu wa Kiislamu waitisha maandamano zaidi

17 Agosti 2013

Mji mkuu wa Misri Cairo ulitumbukia katika ghasia Ijumaa(16.08.2013) wakati watu waliokuwa wakilinda doria katika vizuwizi vilivyowekwa katika vitongoji vya mji huo walipopambana na waandamanaji.

A protester supporting ousted Egyptian President Mohamed Mursi carries an injured demonstrator (R) during clashes outside Azbkya police station at Ramses Square in Cairo, August 16, 2013. About 50 people were killed in protests in Cairo on Friday, security officials said. Thousands of supporters of deposed President Mohamed Mursi have been staging nationwide protests against a security crackdown on Islamists. REUTERS/Amr Abdallah Dalsh (EGYPT - Tags: POLITICS CIVIL UNREST TPX IMAGES OF THE DAY)
Maandamano ya kundi la Udugu wa Kiislamu Agost 16, 2013Picha: Reuters

Waandamanaji wa Udugu wa Kiislamu wanapinga kuondolewa madarakani kwa Mohammed Mursi na ukandamizaji uliosababisha umwagikaji mkubwa wa damu.

Mapigano makali kabisa ya mitaani ambayo hayajawahi kuonekana mjini Cairo katika muda wa zaidi ya miaka miwili ya ghasia yamesababisha kiasi watu 82 kuuawa, ikiwa ni pamoja na maafisa wa polisi.

Mapambano ya silaha

Wakaazi wamekuwa wakifyatuliana risasi na kuashiria mwelekeo mbaya katika mzozo huo, wakati raia ambao walikuwa na bastola na bunduki walipopambana na waandamanaji waliokuwa wakishiriki kile ambacho kundi la Udugu wa Kiislamu ilikiita "siku ya hasira" , iliyozushwa na hasira dhidi ya majeshi ya usalama kuwaondoa kwa nguvu waandamanaji waliokuwa wamekita kambi katika maeneo mawili mjini Cairo siku ya Jumatano na kuzusha mapambano ya nchi nzima ambapo watu zaidi ya 600 walipoteza maisha.

Kundi la Udugu wa Kiislamu linaendeleza upinzani dhidi ya jeshiPicha: Reuters

Helikopta za jeshi zilizunguka hewani wakati wakaazi wakiwa na hasira dhidi ya maandamano ya Udugu wa Kiislamu wakiwatupia mawe na chupa waandamanaji. Pande hizo mbili pia zilifyatuliana risasi, na kuzusha mapambano katika mitaa katika maeneo yanayokaliwa na watu katika vitongoji vya mji huo.

Maandamano zaidi

Udugu wa Kiislamu wakionyesha ukaidi wameitisha wiki ya maandamano nchini Misri kuanzia leo Jumamosi.Majeshi ya usalama na raia kadhaa waliuzingira msikiti wa al-Fateh katikati ya jiji la Cairo katika eneo la Ramses ambako waandamanaji wa kundi la Udugu wa Kiislamu walikimbilia kujisalimisha wakati wa mapambano hayo siku moja kabla.

Waandamanaji wakifyatuliwa mabomu ya kutoa machoziPicha: Reuters

Polisi ya Misri imewakamata watu 1004 wanaosadikiwa kuwa ni waungaji mkono wa kundi la Udugu wa Kiislamu katika siku nzima ya mapambano ya nchi nzima jana , imesema wizara ya mambo ya ndani katika taarifa mapema leo Jumamosi(17.08.2013).

Idadi ya waliokamatwa ikiwa ni wafuasi wa kundi la Udugu wa Kiislamu imefikia 1004, taarifa hiyo imesema , mjini Cairo pekee wakiwa wamekamatwa watu 558. Mapambano hayo yamesababisha zaidi ya watu 80 kupoteza maisha, kwa mujibu wa maafisa na watu waliokuwa wakishuhudia katika eneo lililowekwa la muda la kuhifadhi maiti.

Umoja wa Ulaya kujadili ghasia Misri

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wamezungumza jana Ijumaa (16.08.2013) juu ya haja ya jibu la pamoja la ghasia nchini Misri na kukubaliana kuitisha mkutano wa mawaziri wa mambo ya kigeni wa Umoja huo wiki ijayo.

Maiti zikiwa zimepangwa msikitiniPicha: Reuters/Amr Abdallah Dalsh

Rais wa Ufaransa Francois Hollande na kansela wa Ujerumani Angela Merkel wametoa wito wa kumalizwa kwa ghasia na kuanza kwa majadiliano nchini Misri.

Taarifa ya serikali ya Ujerumani imesema kuwa Merkel amemwambia rais wa Ufaransa Hollande kuwa Ujerumani, moja kati ya mshirika mkubwa wa kibiashara na Misri , itaangalia upya uhusiano wake na Misri kuhusiana na umwagaji damu uliotokea wiki hii.

Hollande pia amejadiliana na waziri mkuu wa Italia Enrico Letta na waziri mkuu wa Uingereza David Cameron kuhusu ghasia nchini Misri.

Kansela wa Ujerumani Angela MerkelPicha: AFP/Getty Images

Saudi Arabia wakati huo huo imeeleza kuunga mkono serikali ya mpito nchini Misri inayoungwa mkono na jeshi, ikisema nchi hiyo ya kifalme inaiunga mkono nchi hiyo katika mapambano yake dhidi ya ugaidi na upinzani, ikilenga kuhusu rais aliyeondolewa madarakani Mohammed Mursi wa kundi la Udugu wa Kiislamu.

Maafisa wa Uturuki wameendelea na ukosoaji wao dhidi ya ukandamizaji waandamanaji , wakati rais wa nchi hiyo Abdullah Gul akisema, kile kinachotokea nchini Misri ni aibu kwa Uislamu na mataifa ya Kiarabu. Uturuki na Misri zimewaita nyumbani mabalozi wao kwa ajili ya mashauriano siku ya Alhamis wakati uhusiano wao ukizidi kuharibika.

Mwandishi: Sekione Kitojo / ape / dpae / afpe

Mhariri: Caro Robi