1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Heynckes: Corona imefichua mabaya katika soka na jamii

Josephat Charo
3 Mei 2020

Janga la virusi vya corona limefichua maendeleo ambayo hayapendekzi katika soka na jamii kwa jumla, kwa mujibu wa kocha wa zamani mwenye haiba kubwa Jupp Heynckes.

Fußball Pressekonferenz FC Bayern München
Picha: picture-alliance/dpa/S. Hoppe

Heynckes ameliambia gazeti la Welt am Sonntag kwamba ubinafsi na uchoyo umeshuhudiwa ukiwa juu ya maadili kama umoja, ubinadamu na mshikamano.

"Tunatakiwa tufikirie na tubadili hisia zetu tena kwa watu ambao wanakabiliwa na hali ngumu," alisema Heynecknes.

Akiangazia kandanda, alijiunga na wale wanaotaka kuweko na ukarimu zaidi akisema: "Ni muhimu kutafuta njia ya kurejea katika hali ya kawaida zaidi. Gharama za uhamisho na mishahara lazima zipunguzwe tena. Hali ilikuwa ovu kinyume na maadili isiyokubalika wakati mwingine."

Heyneckes, mwenye umri wa miaka 74, ni mshambuliaji wa zamani wa timu ya taifa ya kandanda ya Ujerumani. Kama kocha alishinda kombe la mabingwa Ulaya, Champions, akiwa na Real Madrid ya Uhispania na Bayern Munich. Alikuwa kocha kwa misimu mitatu mjini Munich huku ufanisi mkubwa akiupata mwaka 2013 aliposhinda taji la Bundesliga, kombe la shirikisho DFB Pokal na kombe la mabingwa wa Ulaya.

Ligi ya Bundesliga ilisimamishwa katikati ya mwezi Machi kwa sababu ya janga la corona lakini vilabu vina matumaini ligi hiyo itaanza tena mwezi huu, pakisubiriwa idhini kutoka kwa serikali kuu mjini Berlin.

Hasara kubwa iliyopatikana na timu na utegemezi mkubwa wa mapato kutokana na matangazo ya televisheni yameibua mjadala kuhusu maadili katika soka la Ujerumani.

(dpa)

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW