1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Idadi ya waliouwawa katika shambulio la Kabul yaongezeka

27 Agosti 2021

Idadi ya raia wa Afghanistan waliouwawa katika shambulio la bomu nje ya uwanja wa ndege wa Kabul yaongezeka na kufikia 79 huku 120 wakijeruhiwa vibaya

Afghanistan | Kabul Airport nach Explosion
Picha: Saifurahman Safi/Xinhua/imago images

Zaidi ya watu 120 wamejeruhiwa katika shambulio la bomu lililotokea nje ya uwanja wa ndege wa Kabul. Baadhi ya waliojeruhiwa bado wanatibiwa hospitalini huku wengine, wakiwa wamesharejea nyumbani baada ya kupata nafuu.

Wanajeshi wa Marekani wanaosaidia kuwaondoa waafghanistan wanaotaka kuitoroka nchi yao, wako katika tahadhari baada ya shambulizi la jana lililofanywa na kundi la dola la kiislamu lililosababisha pia mauaji ya wanajeshi 13 kutoka Marekani. Taifa hilo limesema liko tayari kukabiliana na mashambulio mengine iwapo yatatokea 

Takriban raia 400 wa Afghanistan waliohamishwa wafikishwa Korea Kusini

Wakaazi wa Kabul wameelezea hofu yao kutokana na shambulio la jana. Hussein anayeishi Magharibi mwa mji wa Kabul amesema amekasirishwa na matukio yanayoendelea nchini mwake na huu ni muda mbaya sana anaopitia maishani mwake.

Amesema baadhi ya watu wanayalaumu makundi ya watu waliokusanyika katika uwanja wa ndege wakisubiri kuondoka, wengine wanailaumu Jumuiya ya Magharibi kukubali watu kuondoa licha ya hali ya mvutano na viurugu iliyopo katika uwanja huo.

Wengine pia walililaumu kundi la Taliban kutoweka mikakati ya kutosha kuhakikisha uwanja wa ndege ni salama.

Washambuiaji walilenga kusababisha mauaji ya wengi

Wakati hayo yakiarifiwa  shirika la kutetea haki za binaadamu la Umoja wa Mataifa limelaani shambulio hilo, likisema ni wazi kuwa waliotekeleza maovu hayo walilenga kufanya mauaji ya watu wengi.

Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia watoto UNICEF pia limelaani mashambulizi hayo likitoa wito wa watoto kulindwa zaidi nchini Afghanistan.

Biden: Tutawaondoa raia wote Afghanistan

Muakilishi wa shirika hilo nchini Afghanistan Herve Ludovic amesema wana wasiwasi wa usalama wa watoto na kuendelea kutokea kwa mashambulizi dhidi ya watoto katika wiki za hivi karibuni.

Kulingana na Umoja wa Mataifa kuanzia mwanzo wa mwaka huu watoto 550 wameuwawa huku zaidi ya 1400 wakijeruhiwa Afghanistan.

Mataifa jirani na Afghanistan yaombwa kufungu mipaka kwa waafghan

Mkuu wa Shirika la UNHCR linalowahudumia wakimbizi Filippo GrandiPicha: picture-alliance/dpa/S. Di Nolfi

Shirika la UNHCR linalowahudumia wakimbizi pia limepaza sauti yake juu ya hali ilivyo Afghanistan. Shirika hilo la Umoja wa Mataifa limesema nusu milioni ya waafghan huenda wakaitoroka nchi hiyo ifikapo mwishoni mwa mwaka huu kukwepa utawala wa kundi la Taliban. UNHCR imetoa wito kwa mataifa jirani kuwacha miapaka yao wazi kwa wale wanaokimbilia mahala salama.

Mkuu wa shirika hilo Filippo Grandi, tayari amekuwa na mazungumzo na rais wa kamisheni ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen na wafadhili wengine juu ya usaidizi wa kifedha kwa shirika hilo, kuanza mara moja mikakati ya kutoa hifadhi kwa wakimbizi.

Wanajeshi wa kigeni wako katika tahadhari baada ya shambulio la IS Afganistan

Katika hatua ya kutafuta suluhu ya matatizo ya watu wa Afghanistan Waziri wa masuala ya kigeni wa Italia Luigi Di Maio amesema kundi la mataifa tajiri na yale yanayoinukia kwa kasi kiuchumi, G20 yanapaswa kuandaa mkutano wa kilele kujadili mgogoro wa Afghanistan.

Di Maio ambayo nchi yake inashikilia urais wa kupokezana wa kundi hilo ametoa tamko hilo leo baada ya kukutana na mwenzake wa Urusi  Sergei Lavrov. Hakuna tarehe iliyopendekezwa ya kuandaa mkutano huo.

Chanzo: ap/reuters/ap/afp

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW