1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

IEBC yaendelea kutangaza matokeo siku tatu baada ya uchaguzi

12 Agosti 2022

Tume ya uchaguzi nchini Kenya inaendelea na mchakato wa kutangaza matokeo ya kinyang'anyiro cha urais kutokea maeneo bunge, baada ya kufanyiwa uhakiki na kujumlishwa siku tatu baada ya uchaguzi kufanyika.

Kenia Wahlen
Picha: Sayyid Abdul mAzim/AP/picture alliance

Kwa mujibu wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka ya Kenya (IEBC),utaratibu unaofuatwa unaegemea awamu nne za kuhakiki matokeo, hii ikiwa ni ishara kuwa mshindi wa urais hayuko mbali na kutangazwa.

Tume ya IEBC imeandaa vitengo vya kutazama viashiria, utaratibu, usimamizi na ubora, ambapo kila afisa msimamizi anayewasilisha fomu za 34A na B analazimika kuyapitia madawati hayo manne kabla ya matokeo kufanyiwa uhakiki na fomu 34C kuandaliwa na mwenyekiti wa tume hiyo, Wafula Chebukati.

Mawakala wa wagombea wa urais wanaruhusiwa kuwa kwenye madawati yote manne kushuhudia kinachoendelea.

Akitangaza matokeo ya mwanzo mwanzo kutoka maeneo bunge, Chebukati alisisitiza kuwa kauli ya mwisho ni ya IEBC.

”Shughuli ya kumtangaza mshindi ni kazi ya tume ya IEBC. Mawakala wanaweza kujumlisha matokeo yao ila kauli ya mwisho ni ya tume ya uchaguzi.”

Fomu za 34A

Maafisa na mawakala wa uchaguzi wakiendelea na kujumuisha matokeo katika ukumbi wa Bomas wa Kenya siku ya Alkhamis, 11 Agosti 2022.Picha: Sayyid Abdul mAzim/AP/picture alliance

Maafisa wasimamizi wa IEBC walitazamiwa kuwasilisha fomu zote siku ya Ijumaa (Agosti 12).

Jumla ya maeneo bunge 290 yalishiriki kwenye uchaguzi mkuu na matokeo yote yanafanyiwa uhakiki kwenye ukumbi wa Bomas of Kenya.

Kufikia usiku wa Alkhamis (Agosti 11), shughuli ya kuchapisha maelezo ya fomu ya 34A kutokea vituo vyote 46,229 vya kupigia kura ilikuwa karibu na kukamilika.

Kwa mujibu wa Katiba ya Kenya, IEBC inapewa wiki moja tangu siku ya kupigwa kura, iwe imeshakamilisha utangazaji matokeo. Kwa hivyo, mwisho ya kumtangaza mshindi wa urais ni 16 Agosti ambayo ni siku saba baada ya uchaguzi mkuu kufanyika.

Mwenyekiti wa ujumbe wa waangalizi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jakaya Kikwete, aliwaambia wanahabari kwamba "uchaguzi ulipita salama".

"Shughuli ya kupiga kura ilikuwa salama na ulikuwako uwazi mkubwa. Hata hivyo iwapo itatokea kuwa matokeo hayatawaridhisha baadhi, basi mahakama zipo na wanaohisi kuonewa wataweza kusaka haki kupitia njia hizo.” Alishauri rais huyo wa zamani wa Tanzania.

Wapiga kura milioni 14 walishiriki kwenye uchaguzi mkuu wa tarehe 9 Agosti kati ya watu milioni 22 waliosajiliwa.

Imetayarishwa na Thelma Mwadzaya, DW Nairobi

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW