1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Imran Khan ataka uchaguzi ndani ya siku sita Pakistan

26 Mei 2022

Waziri mkuu aliyeondolewa madarakani nchini Pakistan, Imran Khan, ameitaka serikali kutangaza uchaguzi mpya ndani ya siku sita kutoka sasa ama aitishe maandamano makubwa ya umma yasiyo kikomo katika mji mkuu Islamabad.

Pakistan Protestmarsch Islamabad | Imran Khan
Picha: Fayaz Aziz/REUTERS

Akizungumza kwenye mkutano uliowakusanya maelfu ya wafuasi wake mapema siku ya Alkhamis (Mei 26), waziri mkuu huyo aliyeondolewa , amedai kuwa wafuasi wake watano wameuawa katika maeneo mbalimbali ya nchi na serikali aliyoita ya vibaraka, akitishia kuendelea na maandamano ya umma hadi matakwa yao ya kuitishwa uchaguzi mpya yatakapotimizwa. 

FE: Maoni 23/24.04 Pakistan after Imran Khan - MP3-Mono

This browser does not support the audio element.

"Leo, watumwa wa Marekani na mafisadi wakubwa kabisa wa Pakistan wanawaogopa wananchi. Wamefungia njia kwa makontena kote Pakistan, wanazuwia watu wetu na wanawakamata watu wetu," alisema Khan.

Ingawa serikali haijasema chochote kuhusu madai hayo, lakini imetuma wanajeshi kulinda majengo muhimu, yakiwemo ya bunge na ofisi ya Waziri Mkuu Shahbaz Sharif, anayeshutumiwa na Khan kuingia madarakani kwa msaada wa kifedha na kimkakati wa Marekani.

Tayari Khan ameshawasili mjini Islamabad na msafara wa maelfu ya wafuasi wake wanaokisiwa kufika 25,000, tayari kwa kile alichosema ni maandamano yasiyo kikomo hadi matakwa yao ya uchaguzi mpya yatakapotimizwa.

Mahakama ya Juu yaruhusu maandamano

Polisi wa Pakistan wakijaribu kuwazuwia wafuasi wa Imran Khan kuvuuka daraja la Lahore kuelekea Islamabad.Picha: Farooq Naeem/AFP/Getty Images

Serikali ya Waziri Mkuu Shehbaz Sharifilikuwa imeapa kuwa ingeliwazuwia waandamanaji kuingia mji mkuu, ikiyaita maandamano yao kuwa ni "jaribio la kuligawa taifa na kuleta machafuko." 

Lakini baada ya kikao cha dharura cha Mahakama ya Juu jioni ya jana, majaji walitowa ruhusa ya maandamano hayo kufanyika kando ya mji wa Islamabad, ingawa Khan alisema angelishinikiza kufika kwenye kitovu vya mji huo mkuu.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Rana Sanaullah, aliwasihi wananchi kutokujitokeza kwenye maandamano hayo, akisema kuwa umma wa nchi hiyo umemkataa mcheza kriketi huyo wa kimataifa aliyegeuka kuwa mwanasiasa.

"Watu wa Pakistan wamechaguwa kusalia majumbani mwao badala ya kuwa sehemu ya maandamano haya ya vurugu. Watu wamekataa moja kwa moja maandamano haya ya kiadui," aliwaambia waandishi wa habari mapema Alkhamis.

Khan alianza vuguvugu lake la maandamano kuelekea Islamabad kutokea mji wa kaskazini magharibi wa Peshawar, iliko ngome yake.

Makabiliano yaliripotiwa kwenye mji wa mashariki wa Lahore, wakati polisi wa kutuliza ghasia walipotumia gesi ya machozi na kuwarejesha nyuma maelfu ya waandamanaji waliokuwa wakirusha mawe wakati wakijaribu kuvuuka daraja kwa ajili ya kupanda mabasi ya kuelekea Islamabad.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW