Inter Milan yatinga fainali ya Champions League
7 Mei 2025
Matangazo
Hiyo ni baada ya kupapatua ushindi mbele ya vigogo Barcelona katika mchezo wa mkondo wa pili wa nusu fainali ulipigwa usiku wa kuamkia leo.
Mtanange huo kwenye dimba la San Sirro mjini Milan ulikwenda hadi dakika za nyongeza, na Inter ikamudu kuibamiza Barcelona bao 4-3.
Matokeo hayo pamoja na yale ya mechi ya mkondo wa kwanza ambayo timu hizo zilitoka sare ya bao 3-3, yalimaanisha Inter ilikuwa imefunga mabao 7 dhidi ya 6 ya Barcelona.
Ushindi huo unaiwezesha Inter Milan kucheza fainali yake ya pili ya Champions League ndani ya kipindi cha misimu mitatu.
Vijana hao wa kocha Simone Inzaghi watasubiri matokeo ya mechi ya leo ya nusu fainali mkondo wa pili kati ya Arsenal na Paris St. Germain kujua timu watakayokutana nayo fainali.