1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yaonya kuziandama benki za Marekani, Israel

11 Machi 2026

Iran imeonya kwamba kuanzia sasa itaziandama benki na taasisi za fedha zenye mafungamano na Israel na Marekani kote Ghuba na Mashariki ya Kati kufuatia mashambulizi dhidi ya benki kuu yake mjini Tehran.

Iran Tehran 2026 | Mashambulizi ya Israel
Moshi ukifuka jijini Tehran baada ya mashambulizi mengine ya Israel dhidi ya Iran siku ya Jumatano (Machi 11, 2026).Picha: Fatemeh Bahrami/Anadolu/picture alliance

Mapema asubuhi ya Jumatano (Machi 11), droni mbili zinazodaiwa kurushwa na Iran ziliangukia karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dubai, ambapo watu wanne walijeruhiwa.

Hata hivyo, shughuli za safari  kwenye uwanja huo ziliendelea kuwa za kawaida, kwa mujibu wa Ofisi ya Habari ya Dubai.

Kabla ya hapo, kombora jengine liliipiga meli iliyobeba makontena kwenye Mlango Bahari wa Hormuz, ambapo moto mkubwa ulizuka na kuwalazimisha mabaharia wake kujiokowa, kwa mujibu wa jeshi la Uingereza. 

Nchini Kuwait, serikali ilisema mifumo yake ya ulinzi wa anga ilikuwa imefanikiwa kuzidunguwa droni nane za Iran.

Nayo Saudi Arabia iilsema iliweza kuzidunguwa droni tano zilizokuwa zinaelekea kwenye visima vyake vya mafuta vya Shaybah.

Mlango wa Hormuz wafungwa

Iran inatajwa kufanikiwa kusimamisha safari za meli za mizigo kwenye Mlango Bahari wa Hormuz, ambako robo moja ya mafuta yote ya dunia kutokea Ghuba ya Uajemi hupitia kuelekea Bahari ya Hindi. 

Picha iliyotolewa na Kamandi ya Jeshi la Marekani ikidai ni meli ya Iran iliyokuwa ikitega mabomu kwenye Mlango Bahari wa Hormuz kabla ya kuripuliwa kwa kombora la Marekani.Picha: CENTCOM/REUTERS

Pia imekuwa ikivilenga visima na mitambo ya kusafishia mafuta kwenye mataifa jirani ya Ghuba, kwa lengo la kuweka mbinyo wa kilimwengu dhidi ya uchokozi ulioanzishwa na Marekani na Israel mwishoni mwa mwezi wa Februari.

Kamandi yake ya pamoja ya kijeshi ya Iran ilisema siku ya Jumatano kuwa benki na taasisi za masuala ya fedha zingelianza kuwa sehemu ya maeneo yatakayoandamwa na mashambulizi yake.

Makao Makuu ya Khatam al-Anbiya ilitowa taarifa hiyo baada ya vyombo vya habari vya Iran kuripoti kwamba mfanyakazi mmoja wa beki mjini Tehran aliuawa kutokana na mashambulizi ya Marekani na Israel.

"Kutokana na mashambulizi haya haramu na yasiyokubalika, adui anatulazimisha kuvilenga vituo vya kiuchumi na benki zenye mafungamano na tawala za Kizayuni na Marekani kwenye eneo hili," Ebrahim Zolfaqari, msemaji wa kamandi hiyo alisema akiwaonya raia kukaa mbali na benki na taasisi zote za kifedha.

Israel yashambulia Tehran, Lebanon

Kwa upande wake, Israel ilisema ilikuwa inaendelea na mashambulizi yake dhidi ya Tehran kufuatia mashambulizi ya Jumanne ambayo wakaazi wa huko waliyaelezea kuwa makubwa kabisa tangu uchokozi uanze. 

Madhara baada ya mashambulizi ya Israel dhidi ya viunga vya mji mkuu wa Lebanon, Beirut, siku ya Jumatano (Machi 11, 2026).Picha: Hussein Malla/AP Photo/picture alliance

Miripuko ilisikika siku ya Jumatano mjini Beirut na kusini mwa Lebanon, ambako Israel ilidai kulilenga kundi la Hizbullah lenye mafungamano na Iran.

Jengo moja katika kiunga cha Aisha Bakar mjini Beirut liliporomoka baada ya mashambulizi hayo, ingawa hadi sasa hakuna taarifa za watu waliouawa.

Kabla ya hapo, mashambulizi kwenye wilaya ya Nabatieh kusini mwa Lebanon yaliwauwa watu watano na wengine wawili waliuawa kwenye wilaya za Tyre na Bint Jbeil. 

Tangu Hizbullah ilipojiunga rasmi na vita vilivyoanzishwa na Marekani na Israel dhidi ya Iran mwanzoni mwa mwezi huu, mashambulizi ya Israel yameshauwa karibuni watu 500 nchini Lebanon, wengi wao wakiwa raia wa kawaida.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW