ISLAMABAD:Tume ya uchaguzi yabadili sheria
17 Septemba 2007Matangazo
Tume ya Uchaguzi nchini Pakistan imetangaza mabadiliko katika sheria za uchaguzi ambayo yatamruhusu rais Pervez Musharraf kuvuka vizuizi vilivyomkabili katika jitihada yake ya kutaka kugombea tena wadhfa wa urais.
Tume hiyo ya uchaguzi imearifu kuwa imekifuta kifungu kilichokuwa kinamzuia rais wa Pakistan kugombea awamu ya tatu.
Vyama vya upinzani vimelalamika na vimesema jenerali Musharraf hafai kugombea tena awamu nyingine ya miaka mitano ya uongozi huku akiendelea kushikilia cheo cha juu jeshini.
Hata hivyo afisa wa ngazi ya juu nchini Pakistan amesema kwamba jenerali Musharraf anapanga kuachia madaraka ya kijeshi.