1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yapeleka wanajeshi wa ardhini Lebanon

1 Oktoba 2024

Jeshi la Israel limesema wanajeshi wake wako kwenye mapambano makali nchini Lebanon baada ya kuanzisha kile linachodai kuwa ni "operesheni maalum ya ardhini" siku ya Jumanne (Oktoba 1).

Wapiganaji wa Hizbullah nchini Lebanon.
Wapiganaji wa Hizbullah nchini Lebanon.Picha: Anwar Amro/AFP/Getty Images

Kuingia kwa wanajeshi wa Israel nchini Lebanon kumevitanuwa vita hivyo baada ya wiki moja ya mashambulizi yake ya anga yaliyouwa mamia ya watu nchini Lebanon.

Operesheni hiyo ya ardhini ya Israel imekuja katika wakati ambapo nchi hiyo imekuwa ikifanya mashambulizi dhidi ya maeneo ya kusini mwa mji mkuu wa Lebanon, Beirut, mji mkuu wa Syria, Damascus, na Ukanda wa Gaza, licha ya miito ya kimataifa ya kuitaka ijizuie kuutanuwa mgogoro huo kikanda.

Israel yashambulia katikati mwa Beirut

01:03

This browser does not support the video element.

Waziri wa Ulinzi wa Israel, Yoav Gallant, ameonya kwamba vita hivyo vitaendelea hata baada ya kuuliwa kiongozi wa kundi la Hizbullah, Hassan Nasrallah.

Wakati huo huo taarifa zimeeleza kwamba mripuko mkubwa ulisikika siku ya Jumanne (Oktoba 1) katika mji mkuu wa Israel Tel Aviv, huku ving'ora vya kutowa tahadhari ya mashambulio ya anga vikizimika.

Hizbullah imedai kuyalenga makao makuu ya Shirika la Ujasusi la Israel (Mosad) kwenye mashambulizi hayo.