1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Israel yatoa pendekezo kwa Hamas kusitisha mapigano kwa muda

23 Januari 2024

Israel imependekeza kwa Hamas kupitia wapatanishi wa Qatar na Misri, kusitisha vita kwa hadi miezi miwili kama sehemu ya makubaliano ya kuachiwa mateka wote wanaoshikiliwa Gaza.

Israel | Tel Aviv
Hamas inashikilia bado zaidi ya mateka 100 wa Israel.Picha: Jack Guez/AFP/Getty Images

Tovuti ya habari kutoka Marekani Axios, imesema Israel, imeipendekezea Hamas kupitia wapatanishi wa Qatar na Misri kwamba itasimamisha mapigano kwa muda wa hadi miezi miwili kama sehemu ya makubaliano yatakayowezeshakuachiwa huru mateka wote wanaoshikiliwa Gaza.

Ripoti hiyo ambayo haikuwataja maafisa wa Israel imesema mpango huo utatekelezwa katika ngazi tofauti, utakaoanza na kuachiwa mateka wa kike, wanaume wenye zaidi ya umri wa miaka 60 na wale walio katika hali mbaya kiafya wanaohitaji msaada wa haraka.

Soma pia: Kundi la Hamas latoa vidio ikionyesha mateka watatu wakiomba usaidizi

Baadae wataachiwa wanajeshi wa kike, raia vijana, wanajeshi wa kiume na miili ya mateka walioaga dunia.

Hata hivyo, maafisa hao wamesema mpango huo pia utatoa nafasi ya kuachiwa huru baadhi ya wafungwa wa Kipalestina wanaozuiliwa nchini Israel.

Pendekezo hilo halijumuishi ahadi za kusitisha vita, lakini litajumuisha wanajeshi wa Israel kupunguza uwepo wao katika miji mikubwa ya Gaza na pole pole kuwaruhusu raia kurejea huko.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW