Italy yaopoa miili 19 ya wahamiaji waliokufa baharini
2 Aprili 2026
Watu 19 wamefariki dunia na wengine 58 kuokolewa baada ya boti ya wahamiaji kuharibika katika Bahari ya Mediterania ikitokea Libya kuelekea Ulaya.
Waliookolewa, wakiwemo watoto watano, walipelekwa katika kisiwa cha Lampedusa nchini Italia, huku watu watatu wakiripotiwa kupotea.
Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji, IOM, wengi wa waliofariki walikufa kwa baridi kali baada ya kukaa baharini kwa siku kadhaa.
Shirika la uokoaji la Sea-Watch limesema vifo hivyo ni sehemu ya ongezeko la ajali baharini, likikadiria zaidi ya watu 100 wamefariki ndani ya siku tatu zilizopita.
Takwimu zinaonyesha kuwa hadi sasa mwaka huu, zaidi ya watu 640 wamepoteza maisha katika njia ya kati ya Mediterania, ikiwa ni miongoni mwa viwango vya juu zaidi katika miaka ya hivi karibuni.