1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je, wagombea wanawake watabadili siasa za Kongo?

Iddi Ssessanga Zanem Nety Zaidi
16 Desemba 2023

Wanawake wamekuwa na uwakilishi mdogo katika siasa za Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, DRC, hadi sasa. Kabla ya uchaguzi mkuu wa Desemba 20, uungwaji mkono kwa wimbi jipya la wagombea wanawake unaongezeka.

Marie Josée Ifoku
Marie Josee Ifoku anatumai kutengeneza njia ya kusonga mbele kwa wagombea wengine wa kike.Picha: Wendy Bashi/DW

Katika mji wa Goma, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, mkazi wa eneo hilo Alexandrine Kisikutila anawahimiza watu wote walio karibu naye kupiga kura katika uchaguzi mkuu utakaofanyika wiki ijayo. Hasa zaidi, kwawagombea wa kike.

"Kama raia wa Kongo niko tayari kupiga kura na kumpigia kura mwanamke," aliiambia DW.

"Sio kwa sababu mimi pia ni mwanamke, lakini kwa sababu ninaamini kuwa wanawake wanaweza kufikia mambo makubwa, kama wanawake kadhaa maarufu duniani walivyothibitisha. Nadhani tunaweza kuendelea kuwa na athari kwa ulimwengu kwa kusaidiana."

Soma pia:Kuelekea kura DRC, vijana watamani ajira 

Wanawake kwa kawaida wamekuwa hawawakilishwi sana katika siasa za Kongo. Lakini sasa, uungwaji mkono kwa wagombea wa kike unaongezeka - hasa katika maeneo yenye migogoro mashariki mwa nchi.

Kazi yenye 'makuu' na 'isiyo salama'

Wapiga kura nchini Kongo wanatarajiwa kupiga kura Desemba 20 kumchagua rais, pamoja na wawakilishi wa mabunge na mabaraza mbalimbali katika ngazi ya mitaa na kitaifa.

Wapiga kura wataka mabadiliko Kongo

02:54

This browser does not support the video element.

Lakini kuingia katika siasa haijawahi kuwa rahisi kwa wanawake, ambao bado wanazuiliwa na vikwazo vya kitamaduni.

Generose Kagheni, mratibu wa shirika la Women Today, ambalo linajishughulisha na utetezi wa haki za wanawake katika jimbo la Kivu Kaskazini, anaamini kuwa haki za wanawake mara nyingi zinakiukwa nchini Kongo kwa sababu hakuna wanawake wa kutosha katika nafasi za kufanya maamuzi.

Soma pia: Kuondolewa vipeperushi vya wagombea kunazusha mvutano Kongo

"Uwakilishi mdogo wa wanawake katika vyombo vya kufanya maamuzi ni sababu kuu inayoathiri uzingativu unaotolewa kwa mahitaji yao mahususi, ugawaji wa rasilimali na hata uundaji wa mageuzi ya kisheria, kijamii na kiuchumi," aliiambia DW.

"Ndiyo maana ni muhimu kuhakikisha kuwa wanawake wanashiriki katika ngazi zote za maamuzi ili waweze kuwasilisha na kutetea haki zao katika jamii yetu yenye mfumo dume."

Kama mgombea katika uchaguzi wa urais, Marie-Josee Ifoku anasema anaelewa ni kwa nini wanawake wengi wanakwepa shinikizo lisilokwepeka la kazi ya siasa.

"Ni ulimwengu mkali na usio na usalama," aliiambia DW. "Ikiwa huna haiba imara, hautafanikiwa katika siasa."

Soma pia: Wapinzani DRC wafanya mazungumzo Afrika Kusini

Ifoku anaongea kutokana na uzoefu. Kama mgombea rasmi wa chama cha Alliance of Elites for a New Congo, alikuwa gavana wa Jimbo la Tshuapa kuanzia 2016-2017 na alikuwa mgombea pekee mwanamke kuwania katika uchaguzi wa urais wa 2018. Lakini licha ya matatizo hayo, ana matumaini kuwa wanawake wengi zaidi watafuata nyayo zake.

"Pamoja na yote, tumeamua kukaidi hofu, kwa sababu lazima ukubali kwamba kuna hofu kubwa nyuma yake, na hiyo inahitaji ujasiri na kuthubutu," alisema.

Kutafuta 'uwezeshaji' na 'maridhiano ya kitaifa'

Kukuza usawa wa kijinsia kote Kongo pengine ni mmoja ya malengo makuu ya wagombea wa kike.

Joelle Bile, mwandishi wa habari na mwanasiasa ambaye anagombea kupitia chama cha Alternative pour un Congo Nouveau (Chama Mbadala kwa Kongo Mpya), alisema wanawake ndio walio katika nafasi nzuri ya kujilinda.

Mgombea Joelle Bile anasema uwezeshaji wa wanawake na maridhiano ya kitaifa ni katika ajenda yake ya kisiasa.Picha: Wendy Bashi/DW

"Kutokana na hadhi yangu kama mwanamke, nadhani ni vigumu kwangu kuachana na ukweli huu muhimu, hivyo niendelee tu kuwaahidi [wapiga kura] kwamba nitakapochaguliwa, nitafanya vizuri zaidi," aliiambia DW.

Soma pia: Wagombea sita wataka mazungumzo kabla ya uchaguzi Kongo

"Lakini pia, sera zitaundwa ambazo zitahimiza kweli uwezeshaji na maendeleo ya wanawake." Mbali ya usawa wa kijinsia, Bile ana mipango mingine kwa nchi yake akichaguliwa.

"Ningeanza kwa kuomba sensa ya watu. Kuanzia hapo tutapata masuluhisho sahihi ya matatizo ya mara kwa mara ya jamii yetu."

Kuelekea kura hiyo, Ifoku pia anafanya mawazo yake kuhusu mustakabali wa Kongo yajulikane.

"Ninapendekeza kuiondoa jamii ya Kongo katika mfumo wa kizamani kuelekea kitu kipya. Tunatetea uelewa pamoja na maridhiano ya kitaifa," alisema.

Huku uchaguzi ukifanyika katika mazingira ya ghasia zinazoendelea za waasi, sera za utatuzi wa mizozo ni kitovu cha kampeni nyingi.

"Tunataka kuwajenga upya na kuwarejesha Wakongo," alisema Ifoku. "Inapaswa kuwa na nguvu, iliojengwa upya na lazima iheshimiwe. Mifagio [inayotumiwa kama nembo ya kampeni] inaashiria mapambano yetu na kujumuisha nguvu. Usafi ni umoja. Ndiyo mpya."

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW