JERUSALEM : Olmert ataka amani na Syria
10 Julai 2007Waziri Mkuu wa Israel Ehud Olmert amemtaka Rais wa Syria Basher al-Assad kuanza mazungumzo ya moja kwa moja ya amani kati ya nchi hizo mbili.
Mazungumzo kati ya Syria na Israel yalivunjika hapo mwaka 2000 bila ya kulipatia ufumbuzi suala la hatima ya Milima ya Golan iliyotekwa na Israel katika vita vya mwaka 1967 na kuitwaa kwa mabavu hapo mwaka 1981 katika hatua ambayo imetangazwa kuwa batili na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.Assad mara kwa mara amekuwa akielezea utashi wake katika kuanza tena mazungumzo na Israel kwa kupitia mpatanishi.
Wachambuzi wa mambo wanasema kwamba Syria inataka kuirudisha mikononi mwake Milima ya Golan hivi sasa kuliko wakati wowote huko nyuma baada ya kulazimishwa kuondowa vikosi vyake kutoka Lebanon miaka miwili iliopita.