1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMali

Jeshi la Mali lapata pigo katika eneo la kaskazini

28 Julai 2024

Jeshi nchini Mali pamoja na washirika wake wa Urusi, jana walipata pigo na hasara kubwa walipokuwa wakipambana na muungano wa waasi wanaotaka kujitenga kaskazini mwa nchi hiyo.

Wanajeshi wa Mali wakishika doria katika mji mkuu wa nchi hiyo, Bamako huku wakaazi wakiwashangilia mnamo Agosti 19,2020
Wanajeshi wa Mali wakishika doria katika mji mkuu wa nchi hiyo, BamakoPicha: AP Photo/picture alliance

Mohamed Elmaouloud Ramadane, msemaji wa muungano wa waasi wa CSP-DPA ambao unajumuisha zaidi kabila la Touareg, amesema kuwa waasi wa kundi la harakati za Azawad wamedhibiti eneo la Tinzaouatene na lile lililoko kusini mwa nchi hiyo la Kidal.

Wanajeshi wa Mali na washirika wake wakimbia adui

Ramadane ameongeza kuwa mamluki wa Urusi na wanajeshi waMali wamekimbia na wengine wamejisalimisha. Pia alionesha video za maiti kadhaa za wanajeshi na washirika wake.

Jeshi la Mali lasema mapigano dhidi ya magaidi yanaendelea 

Lakini kupitia taarifa, jeshi hilo la Mali limesema kuwa wanajeshi wake ambao wamekuwa wakishika doria katika eneo la Tinzaouaten kwa siku tatu, walikuwa wameanza operesheni za kurudi nyuma kutoka uwanja wa vita kati ya Ijumaa na Jumamosi ili kujiimarisha na kwamba mapigano makali bado yanaendelea dhidi ya muungano wa magaidi.