1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la Nigeria laonya dhidi ya ghasia za mtindo wa Kenya

26 Julai 2024

Vikosi vya jeshi la Nigeria na idara ya usalama ya DSS vimeonya dhidi ya ghasia za mtindo wa Kenya katika maandamano yanayopangwa kufanyika wiki ijayo, kuhusiana na kupanda kwa gharama za maisha.

Nigeria | Proteste gegen Inflation
Picha: SAMUEL ALABI/AFP

Wakati Kenya imekumbwa na maandamano ya maafa yalioilaazimu serikali kuachana na mpango wa kuongeza kodi, Nigeria imeshuhudia vurugu ndogo kuhusiana na mageuzi yake ya kiuchumi ambayo tayari yamesababisha ongezeko la asilimia 40 la mfumuko wa bei za chakula.

Hashtag ya #EndBadGovernanceinNigeria imekuwa ikisambaa kwenye mtandao wa X sambamba na ile ya #RevolutionNow, zikitoa miito kwa Wanigeria kuingia mitaani kuanzia Agosti 1 kunadamana. Lakini haijulikani wazi nani hasa anahusika na miito hiyo ya maandamano. Pia haiko wazi iwapo miito hiyo ya mtandaoni ya kuandamana itawahamasisha watu kuitikia katika wakati ambapo Wanigeria wengi wanapambana na maisha, wakiwa na wasiwasi wa kupoteza ajira zao na wakichukuwa tahadhari kuhusiana na ukandamizaji uliopita.

Nigeria kuendelea na mageuzi ya kiuchumi

Wanigeria wanapambana na mzozo mbaya zaidi wa gharama za maisha katika kipindi cha miaka kadhaa, baada ya Rais Bola Ahmed Tinubu kusitisha mpango wenye gharama kubwa wa ruzuku ya mafuta na kuondoka vikwazo vya ubadilishanaji wa sarafu ya naira, katika mageuzi yaliohitajika ili kufufua uchumi wa taifa hilo lenye watu wengi zaidi Afrika. Miito ya maandamano hayo imekabiliwa na mkururo wa maonyo kutoka kwa maafisa wa serikali, vikosi vya usalama na magavana wakiwahimiza vijana kujitenga nayo. Baadhi wamewashtumu waandaji kwa uhaini na kujaribu kuivuruga nchi.

Msemaji wa Jeshi asema raia hawana haki ya kuhamasisha machafuko

Picha: David Cliff/NurPhoto/picture alliance

Msemaji wa jeshi la Nigeria Meja Jenerali Edward Buba, aliwamabia waandishi habari mjini Abuja kuwa wakati raia wanayo haki ya kuandamana kwa amani, hawana- haki ya kuhamasisha machafuko na kufanya ugaidi. Aliongeza kuwa ni rahisi kuona kwamba muktadha wa sasa wa maandamano yanayopangwa ni kufanya yanayotokea nchini Kenya, ambayo alisema ni vurugu.

Idadi ya Huduma za Taifa, DSS, ambayo inashughulikia vitisho vya ndani, pia ilionya dhidi ya vurugu, ikisema watu wenye nia mbaya walitaka kutumia vibaya maandamano hayo na walikuwa na malengo ya kisiasa. Katika taarifa yake DSS ilisema wapanga njama wanatamani kutumia matokeo ya vurugu ya maandamano hayo kuipaka serikali kuu na serikali za majimbo, kuzifanya zisipendwe na kuzipambanisha na raia.

Rais Tinubu akabiliwa na vihunzi lukuki katika safari yake ya mageuzi

Rais Tinubu, ambaye mara kwa mara ametawaka Wanigeria wawe wavumilivu kwa mageuzi kufanya kazi, siku ya Jumatano walisihi waandamanaji kuwa watulivu ili kuiruhusu serikali kujibu malalamiko yao yote. Yeye pia alisema baadhi ya makundi yalikuwa yanahamasisha maandamano ili kufanya vurugu na kurudufu maandamano ya karibuni nchini Kenya.

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW