1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la Ukraine kuendelea kuutetea mji wa Bakhmut

6 Machi 2023

Licha ya kulemewa vibaya na Urusi katika mji wa mashariki wa Bakhmut, Ukraine imeamua kuendelea kuutetea mji huo hadi dakika ya mwisho, huku waziri wa ulinzi wa Urusi akitembelea mji uliosambaratishwa wa Mariupol.

Ukraine | ukarainische Soldaten nahe der Stadt Bachmut
Picha: Aris Messinis/AFP/Getty Images

Makamanda wa ngazi za juu wa jeshi la Ukraine waliunga mkono kuendelea kuulinda mji wa Bakhmut, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na ofisi ya Rais Volodymyr Zelensky siku ya Jumatatu (Machi 6). 

Rais huyo alikuwa na mktutao na makamanda hao, ambao kwa kauli moja walisema wanajeshi wao wanapaswa kuendelea kuupigania mji huo wenye utajiri wa madini ya chumvi na viwanda vya mvinyo. 

Mkuu wa majeshi, Valeriy Zaluzhnyi, na kamanda wa majeshi ya ardhini, Oleksandr Syrskyi, walizungumzia uungaji mkono wao kwa uamuzi huo, kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa kwenye tovuti ya Ikulu ya Ukraine. 

Soma zaidi: Mkuu wa Wagner aonya juu ya Urusi kushindwa Bakhmut
 

Msimamo huu wa Kyiv ulikuja siku mbili tu baada ya mkuu wa kundi la mamluki wa kijeshi la Wagner kumtaka Rais Zelensky awaamuru wanajeshi wake waliosalia Bakhmut "kuacha mapigano na kuondoka, akidai kuwa kilichosalia sasa ni wazee na watoto wachache ambao walikuwa na siku chache za kuishi."

Mwanajeshi wa Ukraine akiwa amejeruhiwa.Picha: Oleksandr Ratushniak/REUTERS

Mashambulizi dhidi ya Bakhmut yaendelea

Jeshi la Urusi limeendelea kuushambulia mji huo ulio kweye jimbo la Donetsk na vijiji vyake vya karibu, huku maafisa wa huko wakisema Moscow inatumia rasilimali na wanajeshi wengi zaidi kuliko kawaida ili kukomesha kabisa upinzani wa wanajeshi wa Ukraine waliosalia.

Hata hivyo, Bakhmut haina umuhimu wowote wa kimkakati, lakini wachambuzi wanasema ni umuhimu wake ni kisaikolojia kwa Rais Vladimir Putin anayetaka kuutumia ushindi wa jeshi lake kwenye mji huo kutangaza habari njema nchini mwake. 

Soma zaidi: Scholz, Biden waapa kuendelea kushirikiana kuisaidia Ukraine

Kwa upande wa Ukraine, kuendelea kupambana kunamaanisha kutuma ujumbe kwa Moscow kwamba hata baada ya mwaka mzima wa uvamizi, bado inaweza kusimama mbele ya dola kubwa kijeshi kwa msaada wa washirika wake wa Magharibi.

Mwanajeshi wa Ukraine akichimba handaki mjini Bakhmut.Picha: Oleksandr Ratushniak/REUTERS

Akiwa ziarani nchini Jordan hivi leo, Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Lloyd Austin, ameunga mkono mtazamo huo akiongeza kuwa hata kama jeshi la Ukraine litashindwa mjini Bakhmut, hakutakuwa na maana yoyote kwenye uwanja wa kivita. 

Shoigu aitembelea Mariupol

Uamuzi wa Ukraine kuendelea kuutetea mji huo ulikuja wakati Waziri wa Ulinzi wa Urusi Sergei Shoigu akiutembelea mji uliosambaratishwa vibaya kwa vita wa Mariupol kusini mwa Ukraine siku mbili baada ya kuitembelea Bakhmut. 

Soma zaidi: Waziri wa Ulinzi wa Urusi atembelea mstari wa mbele wa vita

Kwa mujibu wa wizara ya ulinzi, ziara hiyo ya Shoigu ilikuwa na lengo la kujionea mwenyewe kazi inayofanywa na Urusi kurejesha tena miundombinu iliyobomolewa vibaya kwenye jimbo zima la Donbas.

Shoigu amekuwa akikosolewa sana nchini mwake kwa kutokuonesha uongozi madhubuti wa kijeshi tangu Urusi ilipoamua kuivamia Ukraine mwishoni mwa mwezi Februari mwaka jana.

Vyanzo: Reuters, AFP

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW