1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi nchini Burkina Faso latangaza kurejesha Katiba

Sylvia Mwehozi
1 Februari 2022

Jeshi la Burkina Faso limetangaza kurejesha katiba, wiki moja baada ya kutwaa mamlaka katika taifa la ukanda wa Sahel. Tangazo hilo limetolewa katikati mwa mazungumzo baina yake na wapatanishi wa kimataifa.

Burkina Faso | Paul-Henri Sandaogo Damiba
Picha: Facebook/Präsidentschaft von Burkina Faso

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ghana ambaye anaongoza ujumbe wa Jumuiya ya kiuchumi ya nchi za Afrika magharibi ECOWAS Shirley Ayorkor Botchway, amesema mazungumzo ya mjini Ouagadougou na viongozi wa kijeshi "yalikuwa ya kweli" na kwamba viongozi wa kijeshi walionekana kuyapokea mapendekezo yaliyotolewa, akiitaja kuwa ishara nzuri. Mjumbe huyo amekutana na kiongozi wa mapinduzi Luteni kanali Paul-Henri Sandaogo Damiba na wanachama wengine wa jeshi.

"Burkina Faso sasa ni mwanachama aliyesimamishwa, ECOWAS bado itaendelea kufanya kazi na Burkina Faso. Mapambano, hali ya usalama, ni mambo yanayoathiri Afrika Magharibi nzima na hata nje ya Afrika Magharibi, kuelekea Afrika ya Kati. Na hivyo sisi hatutoiacha Burkina Faso peke yake, tutaendelea kushirikiana na Burkina Faso kupambana na tishio hili la ugaidi, migogoro ya silaha na kadhalika. Kwa hiyo tutafanya kazi na utawala mpya."

Mazungumzo hayo pia yalihudhuriwa na mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa katika nchi za Afrika Magharibi na ukanda wa Sahel UNOWAS, Mahamat Saleh Annadif ambaye pia ameyataja kuwa yenye matumaini.

Shirley Ayorkor Botchway mjumbe wa ECOWAS katika mazungumzo ya Burkina FasoPicha: Alexander Zemlianichenko/AP Photo/picture-alliance

Juhudi hizo za mazungumzo zinakuja muda mfupi baada ya Umoja wa Afrika kusimamisha uanachama wa Burkina Faso kufuatia mapinduzi ya Januari 24. ECOWAS nayo ilisimamisha uanachama wa taifa hilo tangu siku ya Ijumaa na kuonya juu ya uwezekano wa vikwazo kulingana na matokeo ya mazungumzo na viongozi wa kijeshi.

Mapema siku ya Jumatatu, katika taarifa iliyotolewa kupitia televisheni, jeshi lilitangaza kuwa limeidhinisha "kitendo cha msingi" kinachoondoa kufutwa kwa katiba. Jeshi hilo, limelitaja rasmi Vuguvugu la Wazalendo la MPSR  kuwa litaendelea kuhakikisha utulivu wa nchi likisubiri kuanzishwa kwa kipindi cha mpito. Hata hivyo halikutoa muda wa kipindi hicho, lakini limemtambua kamanda wa kijeshi Damiba kuwa rais wa MPSR na kiongozi mkuu wa kijeshi.Jeshi Burkina Faso lakemewa licha ya uungwaji mkono

Aidha wajumbe wa ECOWAS waliweza kumtembelea rais aliyeondolJeshi Burkina Faso lakemewa licha ya uungwaji mkonoewa madarakani Roch Marc Christian Kabore ambaye bado yuko kizuizi cha nyumbani. Viongozi wa jumuiya hiyo watafanya mkutano wa kilele mjini Accra Ghana siku ya Alhamis, ili kutathmini matokeo ya mazungumzo na viongozi wa jeshi na kuamua ikiwa watatangaza vikwazo dhidi ya Burkina Faso. Katika kipindi cha nyuma ECOWAS ilisimamisha na kutangaza vikwazo dhidi ya wanachama wake wawili Mali na Guinea ambazo zote zimeshuhudia mapinduzi ya kijeshi ndani ya miezi 18 iliyopita.

Mnamo Januari 24, wanajeshi walimzulia Kabore huku kukiwa na hasira ya umma kutokana na kushindwa kwake kukomesha ghasia za wanajihadi zinazoharibu taifa maskini la Sahel.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW