Merz aelekea China kwa mazungumzo na Rais Xi Jinping
24 Februari 2026
Wolfgang Niedermark mwanachama wa bodi ya Shirikisho la viwanda vya Ujerumani (BDI) amemtolea wito Merz kushughulikia waziwazi masuala kama vile uwezo kupita kiasi, upotoshaji kwenye ushindani na udhibiti wa mauzo ya nje ya malighafi muhimu.
Amesema ni wazi kwamba kampuni za Ujerumani na Ulaya haziko tu katika ushindani wa kibiashara na makampuni makubwa ya China lakini pia yapo katika ushindani ya kimifumo iliyoundwa na mataifa tofauti. Niedermark amesema bila ya mabadiliko upande wa China, mivutano mipya ya kibiashara na Umoja wa Ulaya huenda ikatokea.
Amesema udhibiti wa madini adimu ya China yanatishia usalama wakiuchumi wa Ulaya huku taratibu za leseni zisizo wazi na ufikiaji wa soko teule zikipotosha zaidi ushindani na kuathiri maamuzi ya uwekezaji.
Merz anaondoka leo Jumanne kwenda China kwa ziara yake ya kwanza tangu alipokuwa kansela mwaka uliopita.
Ziara ya Merz itaugusia pia mgogoro wa Urusi na Ukraine
Siku ya Jumatano atakutana na Rais Xi Xinping mjini Beijing na miongoni mwa mambo watakayoyajadili pia ni masuala ya kiusalama ikiwemo mgogoro wa Urusi na Ukraine ambao umeingia mwaka wake wa nne hii leo Februari 24, 2026. Mengine yatakayojadiliwa ni ushirikiano wa kiuchumi wa na China.
Kansela huyo wa Ujerumani pia anatarajiwa kujadili masuala ya haki za binaadamu nakuutembelea mji maarufu wa Forbidden City" huko huko mjini Beijing. Katika ziara yake ya China Merz ameandamana na ujumbe wa biashara na pia atalitembelea jiji la kibiashara la Hangzhou.
Uchumi wa Ujerumani unaoongozwa na mauzo ya nje, umekuwa ukitegemea zaidi soko kubwa la China katika miaka ya hivi karibuni, lakini pia mauzo ya bidhaa za Ujerumani kama vile magari yamepungua kutokana na ushindani wa ndani unaoongezeka. China ilikuwa mshirika mkuu wa biashara wa Ujerumanimwaka wa 2025, ikiipiku Marekani kutokana na sera za ushuru za Rais Donald Trump.