1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kimbunga Beryl chaipiga Jamaika na sasa kinaelekea Mexico

4 Julai 2024

Kimbunga Beryl kimeleta maafa makubwa kwenye mataifa ya kanda ya Karibia baada ya kuipiga Jamaica, Barbados na kuharibu kiasi asilimia 95 ya makazi ya watu kwenye taifa la visiwa la St. Vincent na Grenadines

Kimbunga Beryl
Kimbunga Beryl kimeipiga Jmaica na kuharibu makaziPicha: AP Photo/picture alliance

Kimbunga Beryl kimeleta maafa makubwa kwenye mataifa ya kanda ya Karibia baada ya kuipiga Jamaica, Barbados na kuharibu kiasi asilimia 95 ya makazi ya watu kwenye taifa la visiwa la St. Vincent na Grenadines. Hadi sasa watu 9 wamekufa na inaelezwa Kimbunga hicho kimeanza kubadili mwelekeo na sasa kinatazamiwa kitaipiga pwani ya Mexico.

Soma zaidi.Kimbunga Beryl chaipiga Jamaika 
Taarifa kutoka kanda hiyo zinasema kimbunga Beryl kinaelekea pwani ya Mexico hii leo baada ya kusababisha madhara kwenye mataifa ya visiwa vya kanda ya Karabia. Usiku wa kuamkia leo kimbunga hicho kilitarajiwa kuwasili visiwa vya Cayman kabla ya kuelekea mwambao wa pwani ya Mexico. 

Maji yamefurika katika maeneo ya ufukweni nchini JamaicaPicha: VICTOR GONZALEZ/AFP/Getty Images

Kulingana na Kituo cha Kitaifa cha kufuatilia Vimbunga cha nchini Marekani (NHC) makali ya kimbunga hicho yalipungua kufikia ngazi ya tatu ya ukubwa katika kipimo kinachotumiwa kupanga kitisho cha vimbunga.

Hapo jana, kimbunga Beryl kiliipiga Jamaica kiking'owa miti, kuezuwa mapaa na kuharibu mashamba huku visiwa kadhaa vya eneo la Karibia vikikabiliwa na pepo kali na mafuriko makubwa kwa siku kadhaa sasa. 

Soma zaidi. Idadi ya vifo kutokana na mafuriko Kenya yaongezeka hadi 228

Akitoa taarifa fupi juu ya kimbunga hicho Mkurugenzi wa Kituo cha Taifa kinachoshughulikia masuala ya vimbunga nchini Jamaica alisema: 

"Tunaona baadhi ya ripoti za redio za kuhusu uharibifu, uharibifu unaotokana na upepo, mawimbi ya dhoruba yanayotokea katika mkondo huu wa pwani ambapo tunaona pepo hizi za kusini na kusini mashariki katika pwani ya kusini ya Jamaika. Tunatarajia kuona mawimbi yenye dhoruba ya futi 6 hadi 9 juu ya viwango vya kawaida.Mawimbi hatari. Kwa hivyo hali hatari inayoendelea Jamaica itaendelea kwa saa kadhaa zijazo. Kila mtu anatakiwa kukaa mahali pa kujikinga siku nzima, hadi usiku wa leo.”

Kimbunga Beryl kimesababisha mgagano wa meli za wavuviPicha: FRANCESCO SPOTORNO/AFP/Getty Images

Serikali nchini Jamaica imetayarisha makazi 112 yenye uwezo wa kuchukua watu 20,000. Shule katika jimbo la Quintana Roo zimesimaishwa kwa muda na zaidi ya watu laki nne wakiachwa bila umeme kutokana na kimbunga hicho.

Kimbuga Beryl kinaelekea Mexico

Mbali ya Jamaica, taifa jingine la kisiwa la Barbados nalo lilishuhudia hasira za kimbunga Beryl. Boti ziligongana na kuharibika kwenye maeneo ya ufukweni na miundombinu kadhaa hasa barabara iliharibiwa. Maafa zaidi yametokea kwenye taifa la visiwa la St. Vincent na Grenadines ambapo asilimia 95 ya makazi ya watu yamesambaratishwa kwa upepo mkali au maji yaliyofurika kutokana na kimbunga.

Soma zaidi. Upepo mkali na mvua kubwa yashuhudiwa pwani ya Tanzania

Maafisa wamesema watu watatu wamepoteza maisha huko Grenada na Carriacou, mtu mmoja huko St. Vincent na Grenadines huku vifo vingine vya watu watu watatu vimeripotiwa kaskazini mwa Venezuela na wanne wakiwa hawajulikani walipo.

Maafisa wa polisi wakisafisha barabara baada ya kuathirika na kimbungaPicha: Marco Bello/REUTERS

Katika wakati kimbunga hicho kinaelekea Mexico mmamlaka nchini humo zimeanza kuchukua hatua za kukabiliana na kimbunga hicho kwa kuzihamisha baadhi ya jamii zilizopo katika maeneo ya ufukweni.

Jeshi la Wanamaji la Mexico sasa limeshika doria katika maeneo kama vile Tulum huku likiwahamasisha watalii kujiandaa kuwasili kwa kimbunga Beryl.

Mapema leo asubuhi, Kimbunga hicho kilikuwa umbali wa maili 500 sawa kilomita 800 katika upande wa kusini-mashariki mwa ufukwe wa Tulum nchini Mexico.


 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW