1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Uhuru wa vyombo vya habariAmerika ya Kaskazini

Kimmel: Sakata langu limeweka mstari wa uhuru wa maoni

9 Oktoba 2025

Jimmy Kimmel amesema kusimamishwa kwa show yake baada ya shinikizo la utawala wa Trump kumeweka “mstari mwekundu” wa kulinda uhuru wa maoni nchini Marekani. Show yake ilisitishwa kufuatia utani wake kuhusu mauaji ya Kirk

USA Los Angeles | Kipindi cha Usiku “Jimmy Kimmel Live!”
Picha hii iliyotolewa na Disney inamuonyesha Jimmy Kimmel akiendesha kipindi chake cha usiku “Jimmy Kimmel Live!” mjini Los Angeles, Jumanne, Septemba 23, 2025.Picha: Randy Holmes/Disney via AP/picture alliance

Mchekeshaji maarufu wa Marekani Jimmy Kimmel amesema anatumai hasira ya umma kufuatia kusimamishwa kwa kipindi chake cha televisheni baada ya shinikizo kutoka kwa serikali ya Rais Donald Trump imeweka "mstari mwekundu” wa kulinda uhuru wa maoni nchini humo.

Kimmel aliondolewa hewani kwa muda mfupi mwezi uliopita baada ya kutoa maoni kufuatia mauaji ya mwanaharakati wa mrengo wa kulia Charlie Kirk, hatua iliyosababisha ghadhabu kubwa ya wananchi. Baada ya wiki moja, kituo cha ABC kinachomilikiwa na Disney kilirudisha kipindi chake hewani.

"Natumai tumepiga mstari mwekundu mkubwa sana kama Wamarekani kuhusu kile tunachokubali na kile tusichokubali,” alisema Kimmel.

Maandamano ya kutetea uhuru wa kujieleza yalifanyika nchini Marekani kufuatia ya kuondolewa hewani kwa kipindi cha "Jimmy Kimmel Live!”Picha: Brian Cahn/ZUMA/picture alliance

Shinikizo kutoka Ikulu na FCC

Rais Trump amekuwa akikosoa sana utani anaofanyiwa na Kimmel na watangazaji wengine wa usiku, akiwaita "wahalifu wa maoni,” na mara kadhaa amedai vipindi vyao viondolewe hewani.

Kusimamishwa kwa Kimmel kulitokea muda mfupi baada ya mwenyekiti wa Tume ya Mawasiliano ya Shirikisho (FCC), Brendan Carr, kuashiria kwamba leseni za vituo vinavyorusha kipindi hicho zingechunguzwa iwapo havingekitekeleza agizo hilo.

Kimmel alisema maneno yake kuhusu muuaji anayedaiwa wa Kirk yalitafsiriwa vibaya "kwa makusudi na kwa nia ovu” na wanasiasa wa Republican.

Hata hivyo, alitania kuwa, "ningependa kumwalika Trump kwenye show yangu, lakini si lazima Carr.”

Seneta Chris Murphy na wabunge wenzake wakizungumzia uhuru wa kujieleza baada ya Jimmy Kimmel kusimamishwa na ABC kufuatia matamshi yake kuhusu muuaji wa Charlie Kirk.Picha: J. Scott Applewhite/AP Photo/dpa/picture alliance

Kimmel alidhani imekwisha

Akizungumza katika mkutano wa Bloomberg Screentime mjini Los Angeles, Kimmel alikiri kwamba alidhani kipindi chake kingesitishwa kabisa baada ya kampuni kadhaa zinazomiliki zaidi ya vituo 40 tanzu vya ABC kuamua kususia matangazo yake.

"Nilimwambia mke wangu, ‘basi, ndiyo mwisho,'” alisema kwa utani.

Lakini kurejea kwake hewani kuligeuka kuwa hit kubwa ya watazamaji, licha ya kuwa robo ya taifa haikuweza kutazama kipindi hicho kutokana na ususiaji huo.

Chanzo: AFP

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW