Kichapo cha 5-0 dhidi ya PSG chamuondoa De Zerbi Marseille
11 Februari 2026
Klabu ya Marseille, mabingwa mara tisa wa Ufaransa imesema Jumatano kwamba wameachana na kocha huyo kufuatia makubaliano ya pande zote mbili.
Kipigo cha aibu cha Jumapili kwenye uwanja wa Parc des Princes, kiliwafanya mabingwa watetezi PSG kujiimarisha kileleni kwa pointi mbili dhidi ya Lens baada ya mzunguko wa 21, huku Marseille ikiwa nafasi ya nne baada ya kichapo hicho.
"Kufuatia mashauriano yaliyohusisha wadau wote katika uongozi wa klabu - mmiliki, rais, mkurugenzi wa mpira wa miguu na kocha mkuu - iliamuliwa kumbadilisha kongozi wa kikosi cha kwanza," Marseille alisema. "Huu ulikuwa uamuzi wa pamoja na mgumu uliochukuliwa baada ya kuzingatiwa kwa kina, kwa maslahi ya klabu na ili kushughulikia changamoto za michezo ya mwisho wa msimu."
De Zerbi awaomba radhi mashabiki wa Marseille
Kuondoka kwa De Zerbi kunafuatia pia kipigo kingine cha mabao 3-0 dhidi ya Club Brugge, wiki mbili zilizopita, matokeo yaliyoitupa nje klabu ya Marseille kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
De Zerbi, aliyewaomba radhi mashabiki wa klabu hiyo ya Marseille baada ya kichapo cha wapinzani wao wa jadi PSG, alijiunga na Marseille mwaka 2024 baada ya kuifundisha klabu ya Brighton kwa misimu miwili. De Zerbi aliiongoza Marseille na kumaliza nafasi ya pili msimu uliopita.
Marseille iliyotawala soka la ndani mwishoni mwa miaka ya 1980 na mwanzoni mwa miaka ya 1990, haikutangaza mara moja mtu atakayerithi mikoba ya De Zerbi kabla ya mchezo wa ligi siku ya Jumamosi dhidi ya Strasbourg.