Hatua ya makundi yafungwa kwa rekodi, drama na mshangao
28 Juni 2026
Hatua ya makundi ya Kombe la Dunia 2026 imehitimishwa baada ya mechi 72 za kusisimua zilizochezwa kwa siku 17, huku timu 48 zikichujwa na kubaki 32 zitakazowania ubingwa katika hatua ya mtoano.
Mashindano hayo yamefuta hofu kwamba ongezeko la timu lingeathiri ubora wa mchezo. Badala yake, yameshuhudia rekodi mpya, matokeo ya kushangaza na ushindani mkali katika makundi yote.
Mchezo wa mwisho wa hatua hiyo ulimalizika kwa drama kubwa baada ya mshambuliaji wa Austria, Saša Kalajdžić, kufunga bao la kusawazisha 3-3 dhidi ya Algeria katika dakika za mwisho kabisa za muda wa nyongeza.
Bao hilo halikuokoa Austria pekee, bali pia lilihitimisha rasmi hatua ya makundi na kufunga pazia la awamu iliyokuwa imejaa hisia, furaha na majonzi kwa timu mbalimbali.
Mabingwa watetezi Argentina, Ufaransa na wenyeji Mexico walimaliza hatua ya makundi kwa ushindi wa mechi zote tatu na kutuma ujumbe kuwa bado ni miongoni mwa timu zinazopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa.
Messi aendelea kuandika historia
Lionel Messi ameendelea kuthibitisha ubora wake licha ya umri wa miaka 39. Nahodha huyo wa Argentina ndiye kinara wa mabao wa mashindano hadi sasa akiwa na mabao sita.
Mbali na kuwania kiatu cha dhahabu kwa mara ya kwanza, Messi ameweka rekodi ya mabao 19 katika historia ya Kombe la Dunia na kuwa mchezaji wa kwanza kufunga katika mechi saba mfululizo za fainali za Kombe la Dunia tangu mwaka 2022.
Cristiano Ronaldo wa Ureno, mwenye umri wa miaka 41, naye ameandika historia kwa kuwa mchezaji wa kwanza kufunga katika mashinda sita tofauti ya Kombe la Dunia.
Luka Modrić wa Croatia, mwenye miaka 40, pia amejiunga na orodha ya wachezaji wakongwe waliofunga mabao, huku Kylian Mbappé, Ousmane Dembélé, Erling Haaland na Vinícius Júnior wakifikisha mabao manne kila mmoja.
Makipa Unai Simón wa Hispania na Raúl Rangel wa Mexico nao wameonyesha kiwango bora baada ya kumaliza hatua ya makundi bila kuruhusu bao lolote.
Afrika yaweka rekodi mpya
Bara la Afrika limeandika historia kwa kupeleka timu tisa katika hatua ya 32 bora, idadi kubwa zaidi kuwahi kutokea katika Kombe la Dunia.
Cape Verde, inayoshiriki kwa mara ya kwanza, imekuwa moja ya hadithi kubwa za mashindano baada ya kutoka sare na Hispania, Uruguay na Saudi Arabia na kufuzu hatua ya mtoano.
Kipa Vozinha amekuwa mmoja wa nyota wa timu hiyo na sasa anatarajia kukutana na Lionel Messi na Argentina. Amesema kucheza dhidi ya Messi ni ndoto ya kila mchezaji wa soka.
Morocco pia imeonyesha kuwa mafanikio yake ya kufika nusu fainali mwaka 2022 hayakuwa ya bahati. Sare dhidi ya Brazil imeongeza matumaini ya kufanya vizuri zaidi mwaka huu.
Ghana iliizuia England kwa sare ya bila mabao, huku Côte d'Ivoire ikiwapa wakati mgumu Wajerumani kabla ya kufungwa mabao 2-1 katika dakika za mwisho.
Changamoto na drama nje ya uwanja
Licha ya mafanikio ya baadhi ya timu, mataifa mengine yalikumbwa na changamoto kubwa nje ya uwanja. Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo iliwasili mashindanoni huku ikikabiliwa na mlipuko wa Ebola nchini.
Iran ndiyo iliyokumbana na mazingira magumu zaidi. Timu hiyo ililazimika kuhamisha kambi yake kutoka Marekani kwenda Mexico kutokana na mvutano wa kisiasa kati ya Tehran na Washington.
Pia ilikabiliwa na masharti makali ya kuingia Marekani kwa ajili ya mechi zake, kabla ya kuondolewa kwa uchungu baada ya bao lake dhidi ya Misri kufutwa kupitia VAR katika dakika za mwisho.
Kocha Amir Ghalenoei alisema timu yake haikuathiriwa tu na mazingira ya kisiasa, bali pia ilikosa bahati uwanjani.
Mtoano waanza kwa presha mpya
Mashindano pia yameshuhudia rekodi mpya ya mahudhurio ya mashabiki viwanjani, huku karibu mechi zote zikichezwa mbele ya viwanja vilivyojaa.
Paraguay ilipata habari mbaya baada ya Miguel Almirón kuwa mchezaji wa kwanza kutolewa nje kwa kadi nyekundu chini ya sheria mpya zinazokataza kufunika mdomo wakati wa mabishano na mpinzani.
Ujerumani, iliyopata ushindi mkubwa zaidi wa mashindano kwa kuichapa Curaçao mabao 7-1, imefuzu lakini bado haijawashawishi wengi kuwa ndiyo timu ya kutwaa ubingwa.
Sasa hatua ya mtoano inaanza ambapo hakuna nafasi ya kufanya makosa. Timu 32 zilizosalia zitapambana kwa siku 10 zijazo kuelekea fainali ya Julai 19, huku kila mechi ikiwa ya kufa au kupona.
Kama alivyosema mkurugenzi wa michezo wa Ujerumani, Rudi Völler: "Kila kitu sasa kiko hatarini; ama unasonga mbele au unarudi nyumbani."