1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroAfrika

RSF yadai kuudhibiti kikamilifu mji wa El-Fashir

27 Oktoba 2025

Kundi la wanamgambo wa RSF la Sudan limetangaza kuwa limechukua udhibiti kamili wa mji wa El-Fashir ulio kwenye jimbo la magharibi mwa nchi hiyo la Darfur.

Kundi la RSF limedai kuwa limeutwaa mji wa El-Fasher
Wanamgambo wa RSFPicha: Hussein Malla/AP Photo/picture alliance

Taarifa ya kundi hilo imetolewa Jumapili saa kadhaa baada ya kutangaza kuwa linaidhibiti kambi kuu ya jeshi katika mji huo ambao liliuzingira tangu mwezi Mei mwaka 2024.

Taarifa iliyotolewa na kundi la RSF imesema imeutwaa mji huo kutoka mikononi mwa mamluki na wanamgambo, likimaanisha jeshi la Sudan ambalo limekuwa likipambana nao tangu mwaka 2023.

Mji huo mkubwa ndio wa mwisho ambao haukuwa mikononi mwa RSF huko magharibi mwa Darfur na umekuwa haufikiki kwa urahisi kutokana na mapigano makali.

Taasisi inayohusika na kulinda afya na usalama wa watu walioathiriwa na mizozo ya Chuo kikuu cha Yale HRL imethibitisha kupitia picha za satelaiti kuwa wanamgambo wa RSF walisonga mbele kwenye mji huo, hadi katika kambi kubwa ya jeshi na mapigano makali yalitokea.

Video zilizochapishwa Jumapili na wanamgambo hao zimewaonesha wapiganaji wakisherehekea kando kando ya bango lililoandikwa kikosi cha sita wakati picha nyingine za video ziliyaonesha makundi ya watu wakishangilia sambamba na wapiganaji wa RSF.

Wakati kukiwa na mapambano makali, Shirika la kitabibu la Sudan Doctor Network, limesema vikosi vya RSF vimewaua makumi ya watu na kuharibu vituo vya afya jana Jumapili.

Baada ya taarifa za kutwaliwa kwa mji huo , Gavana wa Darfur mwenye mafungamano na jeshi la Sudan  Minni Minnawi  ametoa wito wa kuhakikishiwa  "ulinzi kwa raia" muda mfupi baada ya wanamgambo wa RSF kudai kuwa wameudhibiti mji huo. Minawi ametaka pia hatma ya watu waliolazimika kuyakimbia makazi yao iwekwe wazi.

Amedai pia ufanyike uchunguzi huru kuhusu ukiukwaji na mauaji ya kimbari yaliyofanywa kwa kificho na makundi ya wanamgambo ambao wamekuwa kwenye mapambano makali na jeshi tangu mwezi Aprili mwaka 2023

Guterres aonya hali itazidi kuwa mbaya Sudan

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameonya kuhusu kuendelea kuchochewa kwa mapigano katika mji El Fasher na kuongeza kwamba hali inayoshuhudiwa Sudan  haivumiliki.

Wakaazi walioathiriwa na mzozo nchini Sudan wakiwa katika moja ya hospitaliPicha: ZDF/Arte/DW

Nayo Ofisi ya uratibu wa misaada ya kiutu ya Umoja wa Mataifa OCHA imeripoti kuwa maelfu ya watu wamekwama katika eneo lenye machafuko la El Fasher huku wakikabiliwa na njaa bila huduma za afya chakula na hawana usalama.

Zaidi, mratibu wa ofisi hiyo ya Umoja wa Mataifa Tom Fletcher ametahadharisha kwamba ameshtushwa na kiwango kikubwa cha majeruhi na raia waliolazimika kuyahama makazi yao. Ametoa wito wa kusitisha haraka mapigano na kuruhusu njia salama ili wapate misaada.

Kulingana na Umoja wa Mataifa, watu wasiopungua 300,000 wanaishi katika mazingira hatari kwenye mji wa El-Fasher ambako haufikiki kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa.

 

Ruka sehemu inayofuata Taarifa kuu ya DW

Taarifa kuu ya DW

Ruka sehemu inayofuata Taarifa zaidi kutoka DW