1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

La Liga kurindima tena Juni 11

1 Juni 2020

Ligi Kuu ya Uhispania La Liga itarudia mechi zake kuanzia Juni 11. Vinara Barcelona wataendelea na mchakato wao wa kuliwania taji kwa kupambana na Real Mallorca Juni 13 ila watakuwa ugenini katika mpambano huo.

Lionel Messi in Barcelona 2020
Picha: Imago Images/AFLOSPORT

Mahasimu wao Real Madrid watakuwa wenyeji wa Eibar Juni 14. Javier Tebas ni rais wa ligi kuu huko Uhispania, La Liga.

"Kutakuwa na siku mbili za mechi katika kipindi cha siku nne, hivyo ndivyo itakavyokuwa. Hatujatangaza siku zengine za mechi kwa kuwa tunasubiri utabiri wa hali ya hewa. Kuna siku ambazo hatutacheza kwa sababu mida ya kucheza itakuwa imekaribiana mno na kunahitajika angalau masaa 72 kati ya mechi moja na nyengine. Kuanzia wakati huo hadi Julai 19 ndio kutaamuliwa bingwa wa La Liga, watakaofuzu kushiriki mashindano ya Ulaya na wale watakaoshushwa daraja," alisema Tebas.