Maafisa wa Mali wafukuzwa kutoka nchini Ufaransa
19 Septemba 2025
Vyanzo vya kidiplomasia vimeliambia shirika la Habari la Ujerumani (DPA) kwamba Ufaransa imetangaza hatua za kupigwa marufuku kuwemo kwenye ardhi ya Ufaransa maafisa wawili wa ubalozi wa Mali mjini Paris mnamo siku ya Ijumaa.
Serikali ya Ufaransa pia imesitisha ushirikiano wake na Mali katika harakati za kupambana na ugaidi nchini. Serikali ya Ufaransa imesema hatua zaidi zinatarajiwa kufuata ikiwa raia wake hataachiliwa mara moja.
Maafisa wawili wa ubalozi wa Mali wametakiwa waondoke Ufaransa kufikia Jumamosi.
Mamlaka ya Mali imejibu kwa kutangaza hatua ya kuwafukuza wafanyikazi watano wa Ubalozi wa Ufaransa mjini Bamako.
Serikali ya mpito ya Mali, inayoongozwa na Assimi Goita, imesema watu kadhaa walikamatwa na kuzuiliwa mwezi Agosti baada ya jaribio la mapinduzi na miongoni mwa watu walokamatwa ni raia wa Ufaransa.
Inadaiwa kuwa kundi la maafisa wa kijeshi na raia walijaribu kuipindua serikali ya Mali kwa msaada kutoka nje ya nchi.
Uhusiano kati ya Bamako na mkoloni wa zamani Ufaransa umevurugika na matamshi ya kuiponda Ufaransa yameongezeka katika miaka ya hivi karibuni. Ufaransa ilisimamisha msaada wake wa kijeshi kwa Mali mnamo mwaka 2022.
Kulingana na gazeti la Ufaransa, Le Monde, ushirikiano katika eneo la kukabiliana na ugaidi uliendelea japo kwa msaada wa mdogo kutoka kwa kikosi cha huduma za kijasusi zawizara ya mambo ya nje ya Ufaransa, DGSE , mjini Bamako.
Uasi unaoendeshwa na makundi ya watu wenye misimamo mikali katika eneo la kaskazini mwa Mali na ukosefu wa utulivu wa kisiasa ni mambo yaliyochochea machafuko nchini Mali kwa zaidi ya muongo mmoja ambayo yamesababisha msururu wa mapinduzi ya mwaka 2020 na 2021 ambayo yamewezesha serikali inayoongozwa na jeshi kuingia madarakani.
Uhusiano wa Ufaransa na nchi za eneo la Sahel umekuwa ukizorota katika miaka ya hivi karibuni na matokeo yake serikali za kiraia nchini Mali, Burkina Faso na Niger zimepinduliwa na wanajeshi.
Vyanzo: DPA/RTRE