Maandamano ya hali ya hewa.
13 Desemba 2009Polisi katika mji mkuu wa Denmark, Copenhagen wamewakamata mamia ya waandamanaji waliofanya maandamano wakiwataka viongozi wanaohudhuria mkutano wa Umoja wa Mataifa wa hali ya hewa kupitisha makubaliano ya dharura ya kuhifadhi hali ya hewa. Katika miji mingi kote ulimwenguni, kulifanyika maandamano, kuwapa changamoto viongozi zaidi ya 100 watakaokutana Copenhagen, kupata makubaliano ya haki na dhati, na pia wazisaidie kifedha nchi zinazoendelea kukabiliana na athari za ongezeko la ujoto duniani. Mjini Copenhagen, waandamanaji walivunja madirisha ya maduka na kuwasha moto barabarani, na pia kuwarushia mawe polisi. Maandamano hayo yanakuja wakati mkutano huo wa hali ya hewa unaingia wiki yake ya pili. Wajumbe katika mkutano huo bado wanazozana kuhusiana na pendekezo la kupatikana kwa mkataba wa kimataifa wa hali ya hewa.